Writen by
sadataley
1:51 PM
-
0
Comments
WAZIRI Mkuu, Kassim Majaliwa amesema haridhiki na hali aliyoikuta kwenye
kiwanda cha kutengeneza mbolea cha Minjingu, baada ya kubaini kuwa
wanatumia mifuko yenye lebo ya Kenya wakati mbolea hiyo inazalishwa hapa
nchini.
Kutokana na hilo, Waziri Mkuu amewataka wamiliki wa kiwanda hicho,
waandike barua kwa Rais John Magufuli kabla hajamaliza ziara yake
keshokutwa na apate nakala ya barua hiyo.
Alitoa agizo hilo jana baada ya kutembelea kiwanda hicho kilichopo
wilaya ya Babati akiwa katika siku ya tatu ya ziara yake mkoani Manyara.
Waziri Mkuu amerejea Babati jana akitokea Dar es Salaam ambako alikuwa
na ratiba za kitaifa.
“Nilikuja kukagua kiwanda baada ya kupokea malalamiko kuwa mbolea hii
haikubaliki huko vijijini. Watafiti wameonesha kuwa ikitumika inasaidia
kutoa mazao mengi.
Lakini wakati niko kiwandani nimekerwa kukuta mifuko ya kupakia mbolea
hii ina anuani ya Nairobi, Kenya wakati mali ghafi inatoka Tanzania,”
alieleza.
“Ni kwa nini mifuko hii ina anuani ya Kenya? Hapa tulipaswa tuone anuani
ya Babati! Je, mlipata kibali kutoka serikalini? Tena kuna lebo ya TBS.
Kwa nini Tanzania haionekani? Kwani malighafi iko Kenya? Haiwezekani, ni
lazima uandike barua na uombe radhi kwa Mheshimiwa Rais Magufuli.
Yeye anahimiza ujenzi wa viwanda ndani ya nchi, halafu ninyi mnafanya hivyo?”
Akiwa ndani ya kiwanda hicho, Waziri Mkuu alikuta baadhi ya mifuko ya
mbolea ikiwa imeandikwa: ‘County Government of Bungoma’, ina nembo ya
Serikali ya Kenya, na anuani ikionesha kuwa mbolea hiyo imetengenezwa na
kiwanda cha mbolea cha Minjingu, lakini anuani inasomeka P.O Box 2941 –
00200 Nairobi, Kenbro Industrial Park, Mombasa Road; namba ya simu
+254-20- 6000-970, lakini mifuko hiyo pia ina muhuri wa TBS.
Baadhi ya mifuko ilikuwa ikipakiwa ndani ya lori tayari kwa kusafirishwa
kwenda kwa wateja. Pia alisema atamwagiza Waziri wa Viwanda, Biashara
na Uwekezaji, Charles Mwijage aje hapa na wanasheria wake na wataalamu
kutoka Tume ya Ushindani wa Kibiashara (FCC) ili waje kuangalia hatua
gani zinapaswa kuchukuliwa.
“Kwa staili hii hii, tumeona watu wakinunua kahawa yetu na kwenda
kuipakia upya huku wakiweka lebo za kwao. Leo hii hata Tanzanite pia
inasemwa imetengenezwa India. Hatuwezi kukubali hali hii iendelee,”
alisisitiza.
“Tukiruhusu hali hii, watu watajuaje kuwa mbolea hii ambayo ni first
class duniani kuwa inapatikana Tanzania? Kiwanda chetu, ardhi yetu,
suala la kutangaza nchi yetu kwa kutumia bidhaa zetu litafanikiwa kwa
njia hii kweli?” “Nataka wakati namaliza ziara nipate taarifa ya hili
jambo pamoja na nakala ya barua ambayo imetumwa kwa Mheshimiwa Rais,”
alisisitiza.
Akitoa maelezo kuhusu hali hiyo, Mkurugenzi wa kiwanda hicho, Tosky Hans
alimweleza Waziri Mkuu kwamba wametumia lebo hiyo kutokana na
makubaliano na wanunuzi jibu ambalo Waziri Mkuu hakulikubali na
kusisitiza kuwa anapaswa aombe radhi.
Waziri Mkuu leo anaendelea na ziara wilayani Mbulu ambako atatembelea
Hospitali ya Haydom, kuzungumza na watumishi na kuzindua Shule ya
Sekondari Singland.
Chanzo:Muungwanablog
No comments
Post a Comment