Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Tuesday, July 28, 2015

Michango ya kampeni yawaliza wagombea CCM

Michango ya kampeni za kujinadi kwa wananchi katika majimbo mbalimbali nchini imelalamikiwa na baadhi ya wanachama wa CCM wanaowania kuteuliwa kugombea ubunge. Kutokana na ukali wa michango hiyo, baadhi ya wagombea wamelazimika kujitoa katika mchakato, wengine wakisema hawawezi kumudu kulipa fedha hizo kwa maelezo kwamba ni kiwango kikubwa. Michango hiyo inatofautiana baina ya jimbo moja na jingine. Hata hivyo chama hicho kimesema hakitishwi na wachache wasioridhishwa na uamuzi unaofanywa kwa masilahi mapana ya chama hicho. Akizungumzia malalamiko hayo jana, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema: “Tunaendelea na mchakato wa kura ya maoni. Kila mtu yuko bize na kura, siwezi kuzungumzia watu wachache wasioridhika wakati wengi wanaendelea na utaratibu tuliojiwekea.” Wagombea watatu katika Jimbo la Bukoba Mjini wamelalamikia kuchangia gharama hizo ambazo kwa mujibu wa agizo la Kamati ya Siasa ya Wilaya, kila mmoja anatakiwa kutoa Sh2 milioni hadi ifikapo leo kabla ya kuanza kwa kura za maoni Agosti Mosi. Mmoja wa wagombea hao, George Rubaiyuka alidai kuwa kiasi hicho ni kikubwa na kwamba alikuwa tayari amelipa Sh200,000 huku mgombea mwingine, Dk Anatory Amani akiomba aongezewe muda ili akamilishe malipo hayo. Mgombea mwingine ambaye hajakamilisha malipo hayo ni Mujuni Kataraiya ambaye pia alipendekeza Kamati ya Siasa kuangalia upya kiwango kilichowekwa. Aliyekuwa mgombea ubunge katika Jimbo la Chalinze, Imani Madega amekaririwa akisema hataweza kukamilisha ndoto yake ya kuwatumikia wananchi wa jimbo hilo kutokana na gharama kuwa kubwa. Kadhalika, mgombea ubunge Jimbo la Morogoro Mjini, Simon Berege alisema kikao cha Kamati ya Siasa ya Wilaya kilikutana Julai 21 na kuchanganua gharama za uchaguzi na kila mgombea alitakiwa kulipa Sh6.9 milioni siku hiyohiyo tena zikiwa taslimu. Berege alisema baada ya uamuzi huo aliomba kupewa muda hadi siku ya pili kukamilisha lakini mgombea mwenzake alijitolea kumkopesha jambo ambalo hakuliafiki. “Ninaamini ukubwa wa gharama iliyowekwa na sharti la kutokushiriki kwenye kampeni hizo isipokuwa tu kwa kulipa fedha hiyo yote ama kwa awamu mbili na kuzuia mtu kufika kwenye mikutano ya kampeni kwa usafiri binafsi umefanywa kwa makusudi ili kufanikisha nia ile ya awali ya kuwa na mgombea mmoja,” alisema Berege. Alisema katika mikutano ya kampeni ambayo amekuwa hahudhurii, imekuwa ikitolewa taarifa kuwa amejitoa jambo ambalo si sahihi na kwamba amekuwa akiwasiliana na mkurugenzi wa uchaguzi wa chama akimweleza kuwa anaendelea kufanya jitihada za kutafuta fedha huku akitaka jina lake liendelee kutajwa katika mikutano ya kampeni. Katibu wa CCM Wilaya ya Morogoro Mjini, Kulwa Milonge alisema hakuna mizengwe ya aina yoyote inayofanyika na kwamba chama kinamtambua Berege kuwa ni mgombea kwa kuwa fomu yake imejazwa kwa usahihi. Alisema Berege haonekani katika kampeni za kujitambulisha kwa wanachama na kwamba alipewa muda wa kutafuta fedha zilizotakiwa kwa ajili ya gharama za kampeni hiyo, hawezi kutajwa mpaka atakapoonekana katika kampeni. Kadi feki zalalamikiwa Huko mkoani Mbeya, wagombea ubunge wa jimbo jipya la Busokelo ambalo awali liliitwa Rungwe Mashariki, juzi wakiwa kwenye Kata ya Lufilyo walitaharuki baada ya kukamatwa kwa kadi 900 za CCM zilizodaiwa kuingizwa kwenye kata hiyo kwa lengo la kumpendelea mmoja wa wagombea. Hata hivyo, Katibu Msaidizi CCM Wilaya ya Rungwe, Simon Yawoo alisema kadi hizo zilitolewa kwa wanachama waliokuwa wakizihitaji kwenye kata hiyo na kwamba ni halali. Dk Mahiga alia rushwa Aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya CCM, Dk Agustino Mahiga amekitaka chama hicho na Serikali kushughulikia tatizo la rushwa linalojitokeza wakati wa huu wa uchaguzi kwa uzito unaostahili kwa kuwa vitendo hivyo vinashusha heshima ya chama hicho tawala na kuchafua taswira ya nchi kimataifa. Dk Mahiga ambaye sasa ni mmoja wa makada 13 wa CCM wanaoomba kuteuliwa na chama hicho kugombea ubunge Iringa Mjini, aliwataka wananchi kushiriki katika vita hiyo ya rushwa na ufisadi katika kipindi hiki cha uchaguzi ili kusaidia kuwapata viongozi bora watakaoongoza na kuliletea tija Taifa. Chanzo;mwananchi.co.tz
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment