Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Wednesday, August 6, 2014

Wananchi: Mdahalo umetufunza mengi


Mjumbe wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Profesa Palamagamba Kabudi (kulia) akizungumza kwenye mdahalo wa Katiba, uliofanyika Dar es Salaam jana. Picha na Edwin Mjwahuzi 
Na Waandishi Wetu, Mwananchi
Dar/ Mikoani. Mdahalo wa Katiba ulioandaliwa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere na kurushwa juzi na ITV umeelezwa kuwa uliotoa mafunzo makubwa kwa watu wengi katika maeneo mbalimbali nchini kuhusu mchakato wa Katiba Mpya.
Wakati waliohudhuria mdahalo huo Dar es Salaam walikuwa kila mara wanawakatisha watoa mada kwa makofi na vibwagizo vya “CCM, CCM, CCM” na “Babu, Babu, Babu”, katika mikoa mbalimbali watu walikusanyika katika maeneo mbalimbali ya vijiweni, baa, madukani kusikiliza huku wengine wakibeba redio na simu za mkononi
Mjini Dodoma, wananchi katika maeneo ya Mitaa ya Nyerere Square, Soko la Dk Rehema Nchimbi na viwanja vya Bunge, walishindwa kuvumilia na kujikuta wapiga kelele za juu katika mada iliyokuwa ikitolewa Profesa Palamagamba Kabudi kuhusu umuhimu wa kupata Katiba Mpya.
Moshi
Makundi ya wafanyabiashara, wafanyakazi na wananchi wa kawaida walionekana wakifuatilia mdahalo huo uliomhusisha Mwenyekiti wa iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba na wajumbe wengine.
Wakati mjadala huo ulipoanza tu, watu mbalimbali walionekana kupigiana simu na wengine kutumiana meseji wakihimizana kuufuatilia.
Mmoja wa waliofuatilia, Christopher Shayo ‘Kimeta’, alisema baada ya kumalizika kwa mdahalo huo ameweza kujua pumba ni zipi na mchele ni upi.
“Sijui kama hawa viongozi wa CCM na wajumbe wao wa Bunge la Katiba waliuangalia, lakini kwa kweli wameumbuka mchana kweupe. Upotoshaji wao ulifikia tamati jana,” alisema Shayo.
Mfanyabiashara, Festo Minja alisema ufafanuzi uliotolewa na wajumbe wa Tume unapaswa kuwa dira ya majadiliano kwa wajumbe wa Bunge la Katiba lililoanza jana bila maridhiano.
Bukoba
Mchuuzi, Derick Edmund anayeuza bidhaa karibu na Hospitali ya Mkoa wa Kagera alisema amefahamu mambo mengi baada ya kufuatilia mjadala huo.
Alisema hoja zilizotolewa na Jaji Warioba kutetea Rasimu ya Katiba ndizo zilizomvutia zaidi na kusema kwa mvutano uliopo sasa itakuwa vigumu kupata Katiba Mpya hivi karibuni.

Mkazi wa Bukoba, Fadhili Hamis alisema kilichomshangaza wakati wa akifuatilia mjadala huo ni jinsi wajumbe wa Tume walivyotetea msimamo wao bila kutofautiana.
Alisema pamoja na kuwa hapendelei muundo wa serikali tatu, hoja zilizotolewa na wajumbe hao wakati wa mjadala zilionekana kuwa nzito na alivutiwa zaidi na mjumbe wa Tume hiyo kutoka Zanzibar, Awadh Ali Said.
Kigoma
Mkazi wa Masanga, Kigoma mjini, Alphonce Mbasa alisema kwa ufafanuzi uliotolewa juzi, wabunge wakipitisha maoni ya vyama vyao kwa kisingizio cha wingi ndani ya Bunge la Katiba hayatasaidia kwa vile wananchi wanajua nafasi yao.
Mkazi wa Kijiji cha Kalinzi, Kamsige Kamsige alisema wajumbe wa Tume wameonyesha uzalendo na hawakuwa tayari kuyasaliti maoni ya wananchi waliyoyatoa katika kuandaa rasimu zote mbili za Katiba.
Mwanza
Ofisa Taaluma Mwandamizi wa Chuo cha Usimamizi wa Fedha (IFM), Tawi la Mwanza, Charles Kadikilo alisema pamoja na hoja nyingi zinazojadiliwa katika midahalo mbalimbali ukiwamo wa juzi, bado haoni ufumbuzi wa kupata Katiba mpya, bali kinachofanyika ni kila mtu kutetea upande wake.
Alisema inawezekana kila mmoja akawa yuko sahihi kwa upande wake ila kinachotakiwa ni kukaa sehemu moja katika meza ya maridhiano na kuacha tofauti zao za masilahi binafsi na vyama vyao.
Arusha
Kada wa CCM, Lembrise Sirikwa alisema mdahalo wa juzi umemsaidia kujua mambo mengi ambayo yalikuwa yamejificha... “Nimefuatilia kwa makini mjadala, kweli kuna mengi nimejifunza na kama kweli tunataka katiba bora ni muhimu kuzingatia kujadili Rasimu iliyopo bungeni na si vinginevyo.”
Fundi wa magari, eneo la Sakina, Godi Kweka alisema kati ya midahalo yote ya Katiba iliyofanyika, amevutiwa na mdahalo wa juzi, kwani ulikuwa ni wa kutoa elimu na kuweka kando ubabaishaji ambao umetawala majadiliano juu ya Bunge la Katiba.
“Nilimpenda sana yule Profesa Kabudi, ametupa historia na elimu juu ya Katiba, kweli alichokisema ni muhimu kukifuata kwani Katiba ni ya wananchi na si ya viongozi,” alisema Kweka.
Mkazi mwingine, Julius Nkya alisema mdahalo wa juzi umechelewa kwani ulitakiwa kufanyika mapema kwa kuwa ndiyo umetoa dira ya ambacho kinapaswa kufanyika na ni busara yaliyojadiliwa juzi kufuatwa na wajumbe wa Bunge la Katiba na Serikali.
Iringa
Mfanyabiashara wa Miyomboni, Iringa, Peter Kibona alisema wajumbe wa Tume walitumia fursa hiyo kutoa majibu ya maswali mengi ya msingi kuhusu Katiba Mpya ambayo wanasiasa wanaopingana bungeni hawana majibu yake.
“Sasa tumeelewa kuwa hata kitendo cha kuivunja Tume ya Mabadiliko ya Katiba kabla ya kukamilika kwa mchakato wenyewe kilifanywa kimakosa,” alisema Kibona na kuongeza:
Kwa msingi huo, Katiba haiwezi kupatikana. Wito wangu kwa viongozi, watumie busara au la Bunge la Katiba lisimamishwe yapatikane maridhiano.
Mfanyabiashara wa kanda za muziki karibu na Kituo Kikuu cha Mabasi cha Iringa, Lema Raymond alisema alilazimika kuongeza sauti wakati wa mdahalo huo ili kuwezesha wananchi kupata ufahamu juu ya mchakato wa Katiba mpya.
Imeandikwa na Geofrey Nyang’oro, Mussa Juma, Ngollo John, Jesse Mikofu, Anthony Kayanda, Phinias Bashaya, Habel Chidawali na Daniel Mjema.
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment