Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Sunday, August 31, 2014

Bunge Maalumu giza nene


 Rais Jakaya Kikwete.PICHA MAKTABA 
Na Neville Meena, MwananchiDodoma. Kadiri siku zinavyosogea kitendawili kuhusu hatima ya Bunge Maalumu kimeendelea kuwa kigumu na sasa kinachosubiriwa ni matokeo ya mkutano baina ya Rais Jakaya Kikwete na viongozi wa vyama vya siasa ambavyo ni wanachama wa Kituo cha Demokrasia Tanzania (TCD).
Awali kikao hicho baina ya Rais Kikwete na viongozi hao kilipangwa kufanyika jana mchana, lakini kiliahirishwa hadi leo saa tano asubuhi kutokana na Rais kukabiliwa na majukumu mengine yanayohusiana na ziara yake inayoendelea mkoani Dodoma.
Habari zilizolifikia gazeti hili jana zinasema taarifa ya kuahirishwa kwa kikao hicho ilitolewa juzi usiku kwa wahusika ambao wote ni viongozi wa vyama vya siasa, na kwamba wale walioko Dar es Salaam watasafiri leo kwa ndege maalumu hadi Dodoma ambako watashiriki mkutano huo.
“Mkutano umeahirishwa hadi kesho (leo) saa tano asubuhi na utafanyika hapahapa Dodoma. Ratiba ya Mheshimiwa Rais kwa leo (jana) haikuruhusu kwa hiyo wahusika waliarifiwa tangu jana (juzi) usiku,” kilisema chanzo chetu.
Rais Kikwete anaendelea na ziara yake mkoani Dodoma na jana ilikuwa siku yake ya tatu alipotembelea Wilaya ya Chamwino. Leo baada ya kukutana na viongozi wa vyama vya siasa, Rais Kikwete atalihutubia taifa pale atakapokuzunguza na wazee wa Mkoa wa Dodoma katika Ukumbi wa Chuo cha Mipango.
Matokeo ya mkutano wa Rais Kikwete na viongozi wa vyama vya siasa yanasubiriwa kwa shauku kubwa kwani huenda yakatoa mwelekeo wa nini kinafuata baada ya kuwapo kwa mkwamo wa mchakato wa Katiba, ambao hivi sasa umefikia katika hatua ya Bunge Maalumu.
Licha ya kwamba Kamati za Bunge hilo zimemaliza kazi yake, lakini kuna wasiwasi kwamba kile kilichojadiliwa kitakosa uhalali wa kisiasa kutokana na kutoshirikisha wajumbe ambao ni wanachama wa vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Ukawa walisusia Bunge hilo Aprili 16 mwaka huu kwa madai ya kwamba hawaridhishwi na mambo yanavyokwenda na wameapa kwamba kamwe hawatarejea bungeni kutokana na sababu ambazo hivi sasa zimebadilika tofauti na zile walizokuwa wakizitoa awali.
Awali viongozi hao walikuwa wakidai kwamba walisusia Bunge Maalumu kutokana na CCM kutumia wingi wao kubadili maudhui ya rasimu iliyotungwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, lakini sasa wanasema pamoja na hilo kuendelea na mchakato ni kufuja fedha za umma kwani hakuna uharaka wa kupatikana kwa Katiba mpya.
Badala yake Ukawa kupitia kwa viongozi wao ambao ni wa vyama vya Chadema, CUF na NCCR Mageuzi, wamesikika mara kadhaa wakidai kwamba hivi sasa taifa linapaswa kujielekeza katika mambo muhimu yakiwamo uandikishaji mpya wa daftari la kudumu la wapigakura, maandalizi ya bajeti ya mwisho ya uongozi wa awamu ya nne na maandalizi ya uchaguzi wa serikali za mitaa na uchaguzi mkuu wa 2015.
Kikao cha leo
Kwa kuzingatia mazingira hayo, kikao cha leo kinaweza kisijikite katika kuwashawishi Ukawa kurejea bungeni, bali kuangalia jinsi ya kusitisha Bunge hilo bila kuleta madhara makubwa ya kisiasa kwa pande zote zinazohusika katika mgogoro unaoendelea.
Kumekuwa na mawazo kwamba kwa mujibu wa Sheria ya Mabadiliko ya Katiba Rais hana uwezo wa kusitisha Bunge, lakini baadhi ya watumishi wa umma wanasema kiongozi wa nchi anaweza kutumia mamlaka yake (prerogative powers) alizopewa na Katiba kusitisha kuendelea kwa taasisi hiyo.
“Pengine kuvunja ni tatizo lakini kwa nafasi yake kama Mkuu wa Nchi, Rais anaweza kusitisha Bunge Maalumu maana ni kama anavyoweza kuteua mawaziri, hakuna mahali amepewa ruhusa ya kuwaondoa, lakini huwa akishateua mwingine maana yake yule aliyepo ameondoka,” alisema mtaalamu mmoja wa masuala ya utumishi serikalini na kuongeza:
“Kwa hiyo hilo Bunge yeye mwenyewe ndiye aliyetoa GN ya kulianzisha na wanasema siku alizotoa ni chache kwa hiyo wanataka huyohuyo atoe GN nyingine kuongeza kwa maana ya kufuta ile ya kwanza. Kwa hiyo anaweza kutoa GN ya kusitisha tu na siyo kosa kisheria”.
Wapinzani kwa upande wao wamekuwa wakijenga hoja kwamba hata kama Katiba itapitishwa hakuna fursa ya kupigiwa kura ya maoni kama sheria inavyoelekeza kutokana na muda kutoruhusu.
Mmoja wa viongozi wa Ukawa, Freeman Mbowe aliwahi kuliambia gazeti hili kwamba uandikishaji wa wapigakura katika daftari la kudumu ni kazi inayohitaji muda usiopungua miezi sita, ikizingatiwa kwamba tayari Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) imeshaweka bayana kwamba daftari la sasa halifai.
NEC ilipokutana na vyama vya saisa ilitangaza kwamba uandikishaji mpya wa wapigakura ungeanza kesho, Septemba 1, 2014 lakini hadi jana hakukuwa na dalili zozote za kuanza kwa kazi hiyo.
Changamoto ya muda
Habari kutoka ndani ya Serikali zinasema muda ni moja ya mambo yanayoifanya Serikali kuona umuhimu wa kusitisha Bunge kwani mbali na mambo makubwa ya kitaifa yaliyotajwa, vikao vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Baraza la Wawakilishi vinapaswa kuanza katika muda ambao vinaweza kuingiliana na Bunge Maalumu.

Wakati Bunge la Muungano likitarajiwa kukutana kuanzia Novemba 4, 2014, Katibu wa Bunge Maalumu ambaye pia ni Katibu wa Baraza la Wawakilishi, Yahya Khamis Hamad alisema jana kwamba vikao vyake vilipangwa kuanza katikati ya Oktoba.
Kwa kawaida vikao vya Bunge hutanguliwa na wiki mbili za vikao vya kamati za kudumu na ikiwa ratiba itabaki kama ilivyo basi vitaingiliana na vikao vya Bunge Maalumu ambalo ratiba yake imepangwa kuendelea hadi Oktoba 31.
Awali Bunge Maalumu lilipaswa kukutana kwa siku 60 katika awamu yake ya pili kama zilivyoongezwa na Rais Kikwete Julai 28 mwaka huu na kuchapishwa katika Gazeti la Serikali (GN) namba 254 ya Agosti 1, 2014.
Katika gazeti hilo, Bunge Maalumu lilipaswa kuanza Agosti 5, 2014 na kumalizika Oktoba 4, lakini ratiba rasmi ya Bunge hilo inaonyesha kuwa litamalizika Oktoba 31, baada ya kuhesabiwa kwa siku za kazi tu badala ya siku za kalenda.
Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, Samuel Sitta Jumatatu hadi Ijumaa ndizo kisheria ambazo wajumbe wanapaswa kufanya kazi na kwamba Jumamosi na Jumapili siyo sehemu ya siku 60 zilizoongezwa na Rais.
Kutokana na hali hiyo, kulikuwa na jitihada za kubadilishwa kwa taarifa ya Rais kwenye Gazeti la Serikali ili kuzingatia mabadiliko hayo, lakini hadi jana Hamad alisema walikuwa hawajapokea maelekezo ya ziada tofauti na yale ya awali.
“Bado tunasubiri maelekezo au niseme ufafanuzi kutoka serikalini maana haya mambo ni ya kisheria kwani hadi sasa ile GN ya kwanza bado haijabadilika,” alisema Hamad ambaye pia ni Katibu wa Baraza la Wawakilishi (BLW).
Naibu Spika wa Bunge la Muungano, Job Ndugai alisema kwa jinsi ratiba ya Bunge Maalumu ilivyopangwa lazima itaingilia na shughuli za Bunge la Muungano, hivyo lazima uamuzi ufanywe ili kuepusha adha hiyo.
“Sisi tumeishaliona hilo kwamba ni changamoto, tulikuwa tukijaribu kujadiliana kuona kama baadhi ya vikao vya kamati vinaweza kuanza mapema hapa Dodoma, lakini uamuzi bado haujafanyika mpaka sasa,” alisema Ndugai.
Kwa mujibu wa ratiba ya Bunge la Muungano, kamati zake za kisekta zilipaswa kuanza vikao wiki mbili kabla ambayo ni Oktoba 20 mwaka huu, siku ambayo bado Bunge Maalumu kwa mujibu wa ratiba iliyopo sasa litakuwa bado halijakamilisha kazi yake.
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment