Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Saturday, September 21, 2013

Biashara ya binadamu TZ-2

Dar es Salaam. Pascalina aliyefiwa na baba yake mwaka 1989 na mama yake mwaka 1996 anasema hata alivyojaribu kuhoji kwa bosi wake alijibiwa vibaya; “aliniambia ‘wewe hapa ni mfanyakazi wa ndani sasa kazi yako ni nini ikiwa mtoto wangu afanye kazi mimi nakupa mshahara wa bure humu ndani’ lile jibu ndilo lililoniondoa katika ile nyumba, miezi minne niliyoishi ilikuwa mingi sana kwangu, niliona haina haja ni heri nirudi kijijini,” anasema Pascalina mama wa watoto wawili sasa.
Esther Meshaki kutoka kijiji cha Ibagi, Kata ya Mang’oto wilayani Makete aliunguzwa kwa maji ya moto baada ya bosi wake wa kike kumfumania akitaka kubakwa na baba mwenye nyumba.
“Niliunguzwa kwa maji ya moto kifuani mwaka 1987, nilikuwa nafanya kazi jijini Dar es Salaam, huko nilichukuliwa na baba mmoja aliyekuja huku Makete kwa shughuli za kikazi, alinichukua nikiwa mdogo sana kama miaka 16 hivi wakati huo nilikuwa nimetoka kumaliza elimu ya msingi. Mkewe alinipokea vizuri tu. Nilifanya kazi kwake kwa miaka 10, nikiwa na miaka sita nyumbani kwake mkewe alifariki dunia, niliendelea kumlelea watoto wake na baada ya mwaka mmoja yule baba alioa tena.
“Huyu mke aliyemuoa kilikuwa chanzo, alikuwa hamtunzi mumewe ananipa majukumu yasiyo na msingi mwishowe yule baba akaanza kunitaka kimapenzi, nilimkatalia siku moja usiku mkewe alichelewa kurudi, matokeo yake yule baba aliingia chumbani kwangu na kuanza kunilazimisha nilikataa wakati akiendelea kutaka kunikamata kwa nguvu yule mama aliingia, waligombana na mwishowe nilijua yameisha.
Baada ya wiki moja yule mama alichukua sufuria ya maji ya moto niliyotenga kwa ajili ya ubwabwa na kunimwagia kifuani,” anasimulia.
Esther anasema alipelekwa hospitali na kutibiwa ila alivyopona aliondoka na kurudi kwao Ibagi, “niliondoka lakini yule baba alianza kuwa hanilipi fedha zangu kwa kuwa sikuwa nikikubaliana na matakwa yake, nilirudi na majeraha yasiyo na fedha ya kujitibia,” anasema Esther mwenye watoto sita na mjukuu mmoja.
Wapo waliopotezana na familia
Kuna idadi kubwa ya wazazi huwaruhusu watoto wao kwenda kutafuta kazi za ndani pasipo kujua watakapofikia, hawa mara nyingi hukosa mawasiliano na ndugu zao na iwapo atapatwa na matatizo ni ngumu ndugu kujua.
Monica, 54, anayeishi kijiji cha Ivilikinge Wilayani Makete anasema “Binti yangu aliondoka mwaka 1992 wakati huo alikuwa na miaka 14 tu tangu hapo hakurudi tena mpaka leo, ilifikia hatua tulitaka kufanya matanga ‘arobaini’ kwa kuamini kwamba amekufa baadhi ya ndugu walikataa na kudai kuwa bado wana matumaini kuwa yupo hai.”
Anasema binti yake aliondoka na kundi la wasichana wenzake ambao wanasema waliachana Ubungo, baada ya mtu wasiyemfahamu aliyefika kijijini hapo kutafuta wasichana kwa ajili ya kazi kuwatawanya kwa watu mbalimbali stendi ya Mnazi Mmoja.
“Wenzake walisharudi siku nyingi sana wana watoto wakubwa tu, sasa mimi nasema kila siku mwanangu yupo ila harudi, mpaka sasa nimeshamsahau kabisa machoni mwangu naweza pishana naye nisimtambue,” anasema Monica.
Agnetha Sanga, 34, anasema; “Mimi nimepotelewa na mdogo wangu Zawadi Sanga mwaka 2006, tangu hapo mpaka leo hatujawahi kuonana, kuna kipindi nilisikia kwamba anafanya kazi Mbeya mjini, ila sina hakika kwani sijawahi kumuona tangu usiku huo alipotoroka huku nyumbani.”
Kwahabari zaidi ingia
 http://www.mwananchi.co.tz/habari/-/1597578/2001644/-/11noy2uz/-/index.html
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment