Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Monday, June 24, 2013

     JUBILII YA KKKT YA MIAKA 50 
NA MAENEO MAPYA YA MISSIONI 
KWA MIAKA 50 IJAYO


Na Mchungaji Profesa Wilson Niwagila


Nachukua fursa hii kumshukuru sana Mheshimiwa Askofu Dk. Benson Bagonza kwa kutupanua mawazo na kuona kwa macho ya ndani maeneo mapya ya Misioni ya Kanisa miaka 50 ijayo. Tukizungumzia maeneo mapya ya misioni tuelewe kwamba tunalenga mawazo yetu katika maeneo haya.

 Kwanza:  Misioni ya ndani. Hapa ni kusema kwamba kanisa linahudumia waumini wake, ili waweze kukua na kuwa na Imani thabiti. Ni mahali pa kuhamasisha waumini kufahamu wajibu wao kama wafuasi waaminifu wa Bwana Yesu, wakihudumiana na kuhudumia watu wengine.  Askofu Dk. Bagonza ameweka bayana hali ya sharika zetu kwamba zinatofautiana kitakwimu kimaendeleo na kimapato; kuna sharika tajiri na sharika maskini lakini sharika tajiri hazisikii deni kusaidia sharika maskini.  Hapa kuna hali ya kusahau tulikotoka. Mwanzo wa sharika tajiri zilikuwa katika hali ya umaskini, vyama vya misioni vikatoa fedha kwa kujenga msingi mzuri. Fedha kutoka vyama vya misioni zilikusanywa kutoka sharika na wakristo wenye moyo wa kuhudumia watu wa nchi nyingine. Sasa hapa kwetu Tanzania sharika tajiri zinafanya mambo mengi yenye garama kubwa lakini hazitupii macho kuona sharika zenye mahitaji ya msingi.
       Dhambi kubwa ya kutajirika, ni kutokuwa na nidhamu ya kutumia utajiri kwa manufaa ya maskini.  Ubinafsi ni tunda la uchoyo. Ikiwa sharika tajiri haziwezi kutambua hili basi tujue kwamba ndio mwisho wa kukua kiroho.  Misioni ya ndani inapaswa kuwa na macho kuona mahitaji ya watu wa Mungu, inapaswa kuwa na  masikio kusikia kilio cha uumbaji wa Mungu, inapaswa kuwa na miguu kuondoka pale ilipo na kufika penye tukio, inapaswa kuwa na mikono kutenda yale yote yaipasayo. Kitabu cha Kutoka SURA ya 3:7-10 ni changa moto kwa kanisa kuelewa maana ya misioni ya ndani na nje. Kanisa haliwezi kufaulu kama halifuati sera ya Mungu: KUSIKIA vilio vya watu wa Mungu, KUONA dhuluma, uonevu na mateso ya uumbaji wa Mungu, KUONDOKA na kuelekea kwenye matukio na KUWAJIBIKA kwa njia yoyote ile ili watu wa Mungu na uumbaji wake ufurahie UKOMBOZI wa Mungu.
 Pili: Eneo la Misioni linaweza kuwa misioni nje ya Kanisa.
 Hapa yanaweza kuwa  maeneo ya kijografia kufuata tulivyozoea kwa kuanzisha maeneo mapya. Pamoja na hayo maeneo mapya yanamaanisha  pia kukabiliana na changamoto mpya ambazo hatukuzoea, kwa mfano mfumo mpya wa mawasiliano, lugha mpya, uhusiano kati ya wasomi na watu ambao si wasomi, uhusiano kati ya matajiri na maskini, uhusiano kati ya vyama vya siasa vikiwa na lengo moja la kumhudumia mwananchi bila kupoteza muda mwingi kwa malumbano. Matabaka haya yote yako ndani ya usharika, mchungaji au mwinjilisti atafauluje kuwahudumia hawa wote pamoja wakaweza kujisikia kwamba ni familia moja katika usharika na katika taifa?
    Kanisa linakabiliwa na changa moto kubwa katika kueneza Injili kwa miaka 50 iliyo mbele yetu. Nidhahiri kwamba changamoto hizi  zinaendana na mabadiliko makubwa na ya kasi kwa mujibu wa uvumbuzi mpya wa mambo ya sayansi, utanda wazi na mabadiliko ya tabia ya nchi, tamaduni na mapokeo. Kanisa haliwezi kuzuia mabadiliko haya lakini lazima liwe makini katika kukabiliana na changa moto hizi. Kanisa lina sura mbili kama shilingi; upande mmoja Kanisa limepewa mamlaka ya kufundisha, na upande wa pili Kanisa limeambiwa kwamba ni Mwanachuo. Roho wa Mungu yupo ndani ya Kanisa akielekeza, akiongoza na kufundisha ili kukabiliana na mabadiliko pamoja na changamoto zake. Kuwa mwana chuo ni kusikiliza mwalimu, kufanya kazi za mwalimu, kufanya utafiti ili kubaini mambo muhimu yatakayomsaidia kuwa mwanachuo mahiri wa kuelekeza wengine katika kufaulu mitihani ya maisha. Hapa napenda kusisitiza kwamba maendeleo mazuri ya mwanachuo ni kutopoteza muda alionao, tena ni kubaini kila msaada uliopo kujiendeleza. Bahati nzuri siku hizi mtu unaweza, ukitaka, kujifunza mambo mengi yenye manufaa kwa njia ya mitandao popote pale. Huna haja ya kwenda maktaba iliyo mbali.
       Maendeleo ninayozungumzia si kujenga barabara au kuleta maji na umeme  nyumbani peke yake bali pia maendeleo ya mtu binafsi kujiendeleza kielimu. Elimu si kwa vijana tu bali pia na kwa sisi wazee. Shoka isiponolewa kazi inakuwa ngumu sana, na unakosa mwelekeo na hapo unaambiwa na vijana “mzee umepitwa na wakati”. Miaka 50 iliyo mbele yetu ni miaka ya kunoa akili zetu, kuwa na mawazo mapya ya kukabiliana na changa moto za Karne hii.
        
       Wakati huu wa mabadiliko ni wakati mgumu wa kuelewa mambo vizuri yanayokabili watu wa Mungu. Wakati mwingine serikali, mashirika, Umoja wa Kimataifa hawana majibu sahihi; lakini Kanisa, kama mwanachuo chini ya mwalimu mkuu Roho Mtakatifu, linafundishwa kukabiliana na changa moto zinazogusa maisha ya binadamu. KUTOKA sura ya 3 Musa anaonesha ugumu wa utume wake- Ilikuwa changa moto kali kumkabili Farao, lakini Mungu anamhakikishia kwamba yuko mbele na nyuma yake.

       Askofu Dr. Bagonza aligusia suala la from the centre to the periphery.
       Hili ni suala muhimu sana na la kufanyia kazi hasa tunapoona watu wengi wanakimbia kutoka the periphery to the centre nikimaanisha kutoka vijijini na mikoani na kukimbilia mijini, jambo ambalo linaleta msongamano wa watu na msongo wa mawazo.
       Niruhusu nitoe mfano huu. Miaka 100 iliyopita chama cha misioni kutoka Ujerumani kilichoitwa Bethel Mission kilifanya kazi Usambara, Bukoba na Rwanda. Mbinu yake ya kueneza Injili ili kukabiliana na upinzani wa Dini ya Kiislamu katika Afrika ya Mashariki ilikuwa kuanzisha maduka ya biashara katika kila stesheni walizozijenga kwa makusudi mawili; kwanza waligundua kwamba waislamu ni wafanya biashara wakubwa hivyo ilikuwa rahisi kuwavutia wananchi kwa biashara yao. Bethel Mission nayo ikaleta kivutio cha biashara kwa makusudi ya kuwavutia watu na kuwasaidia wakristo kununua bidhaa kwa maduka ya misioni. Pili ilikuwa njia ya kuwafundisha wakristo nao kuwa wafanya biashara katika sehemu zao vijijini wakiongozwa na Roho wa Mungu, ili biashara yao isiwe ya kupunja watu walio maskini. Kwa njia hii haya maduka sehemu za vijijini yalibadilisha mwelekeo wa mawazo ya kukimbilia mijini kutafuta maisha. Nakumbuka baada ya kuanza kazi ya ualimu huko Magoye, sasa Dayosisi ya Kusini  Kati, nilihitaji Transistor Radio, badala ya kwenda Mbeya au Iringa nilikwenda Bulongwa ambapo mmisionari mmoja alikuwa ameanzisha duka la kuuza bidhaa muhimu, zikiwemo radio, kwa bei nzuri (poa).
       Ninalotaka kusema hapa ni nini? Changa moto tuliyonayo wakati huu ni watu kukimbilia mijini eti kutafuta Maisha. Mbaya zaidi serikali zetu hazifunuliwi kuanzisha miji na kuweka vitega uchumi vijijini; hivyo watu wote, vijana kwa wazee tunakimbilia mijini na sisi tupate uhondo wa miundo mbinu ya miji.
       Wajibu wa kanisa hapa ni upi? Kanisa litake lisitake litakumbana na changa moto hii. Wakristo wengi wataacha vijiji na kuhamia mijini, makanisa yaliyoko mijini yatasongwa na mambo haya:
       Watu wa tabaka mbalimbali na jinsi ya kuwahudumia kikamilifu
       Msongamano wa watu kutokana na ukosefu wa miundo mbinu bora mijini
       Umaskini uliokithiri utaongezeka mijini
       Magonjwa ya kila aina yatalipuka
       Watu wanaohitaji misaada watakuwa wengi na Kanisa ndilo litafuatwa kutoa msaada.
       Kanisa litakosa watumishi bora  vijijini.
       Huko vijijini watabaki wazee ambao hawatakuwa na msaada wa karibu, hivyo kama mijini mambo hayatakuwa mazuri. Sharika zitaendelea kudhoofika na sharika za mijini zitaendelea kuimarika kifedha. Wachungaji wengi watapenda nao kuhamia mijini ili nao wapate mshahara mkubwa badala ya kupewa posho.
       Watu wanapokuwa wengi mijini matatizo mengi yanaibuka, utunzaji wa mazingira unakuwa na matatizo. Nimebahatika kutembelea Indonesia, Sri Lanka na Philipines. Miji hii imekumbwa na utupaji taka. Pale Jakata Indonesia na Manila Philipines kuna milima ya takataka,kwa kuwa watu katika miji hii ni wengi sana, kuna shida ya kupata ajira, hivyo unakuta wakina mama, na watoto wachanga wako kwenye mlima wa takataka wakichambua kila kitu kuona kama kutapatikana chochote. Afya zao zinahatarishwa na uchafu wanaoshika, vyakula kutoka mahoteli vilivutupwa vinaokotwa na kutumiwa kama chakula
       Hali hii imeanza kujitokeza katika miji yetu ya Tanzania. Taka zinatupwa ovyo tena karibu na mito. Mvua zikinyesha basi uchafu pamoja na sumu za kila ainazinatiririka kwenye maji yanayotumiwa na jamii.                                                                                             
       Kazi iliyombele yetu kama Kanisa ni kufanya yafuatayo:
       Kushauri na kukumbusha serikali kuona umuhimu wa kuendeleza vijiji kwa kujenga miundo mbinu muhimu kusudi wananchi nao wafurahie maendeleo na uhuru wao. Hapa nazungumzia shule navyuo, hospitali nzuri zinazotoa huduma bora, makampuni ya kuwekeza, maji na umeme ili wana vijiji nao waanzishe miradi midogo na mikubwa.
       Kuelimisha jamii namna ya kuendeleza mahali walipo huko vijijini wakiungana na serikali.
       Kazi ya  kutetea wanyonge (advocacy).
       Wajibu mkubwa miaka 50 ijayo ni kukaza nguvu katika utetezi na unabii.                     
        Ulimwengu tuliomo na unaokuja ni ulimwengu ambao hauna huruma. Uonevu, ulafi, unyanganyi, dhuluma, mauaji na kujipenda vitazidi kushamiri. Hapa watuwanyonge ndio watazidi kuteseka na kukosa amani. Hivyo ni wito wa Kanisa kujiweka sawa sawa kupambana na hali hii. 
Ahsante kunisikiliza
Mch. Prof. Wilson Niwagila
Josiah Kibira University College of Tumaini University Makumira 

22/06/2013
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment