Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Saturday, August 30, 2014

Rais atumie fursa hii kuleta maridhiano


Rais Kikwete 
Kwamba Rais Jakaya Kikwete muda wowote kuanzia sasa atafanya mazungumzo na viongozi wa vyama vya siasa vyenye wabunge, wakiwamo viongozi wanaounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), hakika ni habari njema ambazo zimewapa wananchi matumaini makubwa. 
Hivi sasa habari hiyo ndiyo gumzo kuu katika kila kona ya nchi yetu na vyombo vya habari, ikiwamo mitandao ya kijamii ambayo imesheheni maoni ya wananchi wanaounga mkono uamuzi huo wa Rais.
Sisi wa Mwananchi tunaungana na wananchi hao kumpongeza Rais kwa uamuzi huo wa busara wenye lengo la kuwaunganisha wananchi waliogawanyika vipandevipande baada ya mchakato wa kupata Katiba mpya kuvurugwa na wanasiasa.
Bila shaka Rais atakuwa ameona mbali na kutambua madhara yanayoweza kusababishwa na kitendo cha Bunge la Katiba kuendelea na mchakato wa Katiba bila kuwapo mwafaka wa kitaifa, kwa maana ya kutokuwapo uwakilishi mpana katika kujadili na kuboresha Rasimu iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Hakuna asiyejua kwamba mwelekeo hasi wa mijadala katika Bunge hilo linaloandika Katiba mpya ndiyo hasa uliowasukuma wajumbe wake kutoka vyama vya Chadema, NCCR-Mageuzi na CUF kususia vikao na kuunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).
Moja ya sababu za kufanya hivyo ni vitendo vya kibaguzi, kejeli, matusi ya nguoni na vitisho kutoka kwa wajumbe wa chama tawala, CCM, ambacho Ukawa wanasema kiliteka mjadala na mchakato mzima kwa kuweka kando Rasimu ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba na kupenyeza yao iliyotayarishwa na chama hicho. Kwa mtazamo wa Ukawa, katiba ambayo itatokana na mazingira hayo haitakuwa ya wananchi, bali itakuwa ya CCM.
Ni jambo la kusikitisha kwamba tangu wajumbe wa Ukawa wasusie Bunge hilo Aprili 16, mwaka huu hawajawahi kusikilizwa na chombo chenye mamlaka ya juu au chombo ambacho hakina masilahi ya moja kwa moja na mgogoro huo.
Wito wao wa mara kwa mara wa kukutana na Rais Kikwete ulibezwa na kupuuzwa na makada wa chama chake ambao walipaswa kumshauri akutane nao ili kupata maridhiano na mwafaka wa kitaifa.
Hii ni kutokana na ukweli kwamba hakuna mahali popote duniani ambako katiba ya wananchi iliyo nzuri na endelevu ilitokana na mazingira ya ghiliba, hadaa na shari kama ambayo tumeyashuhudia katika Bunge hili.
Katiba yoyote nzuri huhitaji mazingira yenye masikilizano, maelewano na kustahiana.
Mazingira ya matusi ya nguoni, uadui, kebehi, dharau, vitisho na hadaa kama ilivyotokea katika Bunge letu la Katiba huzaa chuki, hivyo katiba inayotokana na mazingira kama hayo kamwe haiwezi kukubalika kwa wananchi kwa sababu hupandikiza chuki na hatimaye kusababisha vurugu.
Ndiyo maana tunampongeza Rais Kikwete kwa kuona hilo na kuridhia kukutana na viongozi wa vyama vyenye wabunge kuzungumzia kadhia hiyo.
Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliandaa Rasimu ya Katiba kwa kuzingatia maoni ya wananchi. Bahati mbaya Bunge la Katiba limetekwa na wanasiasa wanaopigania masilahi binafsi.
Ndiyo maana, pamoja na mambo mengine wamekataa uwepo ukomo wa vipindi vyao vya ubunge, wamekataa wapigakura kuwawajibisha wabunge wao na pia wamekataa pendekezo la mawaziri kutokuwa wabunge.
Katika hali kama hiyo, Rais atafanya vyema iwapo atasitisha Bunge hilo hadi mwafaka wa kitaifa utakapopatikana.
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment