Writen by
sadataley
5:17 PM
-
0
Comments
Na Ibrahim Yamola, MwananchiDar es Salaam. Aliyekuwa Mwenyekiti wa Chadema Mkoa wa Tabora, Kansa Mbarouk amejitokeza ‘kupimana kifua’ na Mwenyekiti wa chama hicho taifa, Freeman Mbowe katika uchaguzi wa ndani unaotarajiwa kufanyika Septemba 14.
Mbarouk alirejesha fomu hizo makao makuu ya
Chadema jana mchana huku akikumbana na kizingiti cha kuzuiwa na walinzi
kuingia ndani kurejesha fomu akiwa pamoja na waandishi wa habari na hata
alipotoka nje hakutakiwa kuzungumza na waandishi hao karibu na jengo
hilo.
Ili kuepusha vurugu, Mbarouk alitoka eneo hilo na
kuanza kuzungumza na waandishi wa habari kwa kusema, “Hili ambalo
limenipata kwa kuzuiwa nisipigwe picha wakati nikirejesha fomu nikiingia
madarakani nitahakikisha narejesha usawa ndani ya chama hiki na katiba
inazingatiwa.”
Aliongeza, “Jambo la pili kulifanya nitahakikisha
wanachama wote ndani ya Chadema wanakuwa na haki sawa, hakuna
atakayeonewa na atakayevunja katiba kwa njia zozote zile atachukuliwa
hatua kali, hakuna atakayekuwa juu ya katiba ya Chadema.”
Juzi, Mbowe alikabidhiwa fomu na makada wa chama
hicho na kumtaka awanie tena kiti hicho, ombi ambalo alilikubali na
kufungua milango kwa wanachama wengine ‘kupimana naye kifua’.
“Nafasi bado ipo, anayetaka kupima kifua na mimi
ajitokeze. Tena nawaomba viongozi wangu msizuie fomu kwa anayetaka,”
alisema Mbowe ambaye ameongoza chama hicho kwa vipindi viwili vya miaka
mitano mitano.
Mbarouk alisema, kulingana na katiba ya chama
Mbowe amemaliza muda wake wa uongozi na anatakiwa kukiachia kiti hicho
kiongozwe na mtu mwingine.
“Mimi nimekuwa mwenyekiti wa mkoa (Tabora) kwa
kipindi cha miaka 10 nikaamua kuachia ili wengine waendeleze vivyo hivyo
na Mbowe ameongoza kwa miaka kumi anatakiwa kuachia ngazi, na hii ni
nafasi yangu imewadia kuiongoza Chadema kufika Ikulu 2015,” alisema
Mbarouk.
Huku akisisitiza alisema, “Kauli aliyoitoa Mbowe
ya kusema anayetaka kujipima kifua naye ajitokeze ni ya kuwatisha
wanachama wasijitokeze, lakini mimi siwezi kutishika na ndiyo maana
nimejitokeza kupimana naye kifua na ninajua nitamshinda kwani katiba
ikizingatiwa tu hawezi kunishinda.” Uchaguzi huo utatanguliwa na wa
Baraza la Vijana Taifa la Chadema, (Bavicha) utakaofanyika Septemba 10
huku Septemba 11 ukifanyika wa Baraza la Wanawake (Bawacha).
Hadi dirisha la urejeshaji fomu linafungwa jana
saa 10.30 makada mbalimbali walikuwa wamejitokeza kuwania nafasi hiyo
miongoni ni Daniel Madiba anayewania Mratibu Mhamasishaji taifa wa
Bavicha na wakili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Lutiger Haule nafasi ya
Ujumbe wa Kamati Kuu kupitia Vijana. Haule alisema anataka kuwatumikia
vijana katika kupata haki zao na atatumia nafasi hiyo kuwapigania kwa
nguvu zote katika harakati za kusaka ukombozi wa pili unaominywa na CCM.
Ushindani ndani ya Bawacha unatarajiwa kuwa kati
ya Mbunge wa Kawe, Halima Mdee, Mbunge Viti Maalum, Chiku Abwao na
makada wengine, Lilian Wasira na Sophia Mwakagenda kwa nafasi ya
mwenyekiti.
Katika hatua nyingine, nafasi ya Naibu Katibu Mkuu
Baraza la Wanawake ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Bawacha),
imeendelea kupata wagombea baada ya Aisha Yusuf kuchukua fomu na
kuirejesha kuwania nafasi hiyo.
Akizungumza katika ofisi za chama hicho zilizopo Kinondoni
jijini Dar es Salaam, Aisha alisema kuwa amelazimika kuwania wadhifa huo
kutokana na kuwa na uwezo wa kutosha. “Hivi sasa ukiangalia wanawake
wengi bado wapo nyuma hivyo ni wakati wa kuondokana na dhana hiyo ndiyo
maana nami nimelazimika kuomba nafasi hiyo,” alisema Aisha.
Alisema kuwa tangu alipojiunga na chama hicho
mwaka 2007 amepata uzoefu ikiwamo kuwa Mwekahazina wa Bawacha Kata ya
Saranga hivyo ameomba ngazi ya juu zaidi ili aweze kuwatumikia wananchi
kwa ukaribu.
Aisha alisema kuwa ni vyema wanawake wakatambua
wao ni jeshi kubwa linaloweza kuleta mabadiliko ndani ya Tanzania
akieleza kwamba sasa taifa lina matatizo makubwa hivyo wanawake
wanapaswa kujitokeza kwa wingi na kuchukua fomu ili kuwania nafasi
mbalimbali za uongozi.
“Wanawake ni lazima tuwe jasiri ni lazima
tuondokane na mifumo dume inayotukandamiza hiyo itatusaidia tupate
nafasi za juu za uongozi katika uchaguzi mkuu ujao,” alisema.
Aisha alisema kuwa anaamini kuwa taifa hili
litaweza kupata maendeleo zaidi ikiwa wanawake wengi watapata nafasi
nyingi za uongozi.
No comments
Post a Comment