Writen by
sadataley
5:13 AM
-
0
Comments
Na Goodluck Eliona na Anthony Mayunga
Dar es Salaam. Ziara ya siku tatu ya Waziri Mkuu wa Thailand, Yingluck Shinawatra imemvutia kiongozi huyo na kuahidi kufanya ziara binafsi katika mbuga za wanyama akiambatana na familia yake.
Akizungumza wakati wa kumuaga waziri huyo aliyeondoka nchini jana, Waziri wa Maliasili na Utalii, Balozi Khamisi Kagasheki, alisema ziara ya Shinawatra imekuwa ya mafanikio makubwa kwa taifa.
Alisema kiongozi huyo ameahidi kurudi nchini wakati wowote akipata nafasi.
“Amesema anakwenda lakini atarudi katika ziara ya kibinafsi yeye na mume wake, mtoto wake na ndugu zake na tumemwambia akiwa tayari atufahamishe,” alisema Balozo Kagasheki.
Alisema kutokana na ziara hiyo, Tanzania na Thailand zimekubaliana na kutiliana saini mkataba wa miaka mitatu wa ushirikiano katika kulinda, kuendeleza na kukomesha biashara haramu ya wanyamapori.
Mkataba huo ulisainiwa na Balozi Kagasheki na Naibu Waziri Mkuu wa Thailand Plodprasop Suraswad, aliyeambatana na Shinawatra.
Akizungumzia manufaa ya mkataba huo, Waziri Kagasheki alisema utasaidia taifa kuongeza mapato kupitia sekta ya maliasili kwa kuongeza watalii.
No comments
Post a Comment