Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Wednesday, February 20, 2013


SALAMU YA MWENYEKITI WA CCT-IBADA YA MAZISHI YA HAYATI BABA ASKOFU DKT. THOMAS O. LAISER
(15 FEBRUARI 2013)
“Kwa maana kwangu mimi kuishi ni kristo, na kufa ni faida” Wafilipi 1:21
Jumuiya ya Kikristo Tanzania ina masikitiko makubwa ya kumpoteza kiongozi mahiri, mkweli, shujaa mwenye ujasiri na nabii wa Kanisa aliyetoa mchango mkubwa sana katika maendeleo na Maisha ya Kanisa na Jamii.
CCT inapenda kutoa salamu ya pole kwa mama mjane Mary Laiser na watoto wake; kwa Dayosisi ya Kaskazini Kati na pia kwa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania.
Kiongozi huyu amelitumikia Kanisa lake, CCT, Jukwaa la Wakristo Tanzania na Kanisa zima la Ulimwengu katika nyadhifa na nyanja mbalimbali kwa uwezo na uaminifu mkubwa.
Katika kumkumbuka kiongozi huyu na kuheshimu mchango wake ndani ya CCT na taifa kwa ujumla, CCT inapenda kuweka bayana kwamba Hayati Ask. Dkt. Laiser ametuachia pengo kubwa sana ambalo kuzibika kwake hakutakuwa rahisi hasa ikizingatiwa kuwa sauti yake ya kinabii imekuwa ikihitajika sana katika vipindi vingi na hasa wakati kama huu ambao umegubikwa na changamoto nyingi zinazohatarisha amani, mshikamano, utulivu na umoja wa kitaifa.
Ili kumuenzi na kumheshimu Hayati Askofu Dkt. Thomas Laiser, CCT inatamka bayana mambo yafuatayo:
1.    Ziko dalili za wazi zinazoonyesha kuwa  wakati huu Kanisa katika Tanzania limeingia kwenye kipindi cha mateso ya wazi ambayo yamejidhihirisha katika matendo ya uchomaji wa makanisa, kutishia usalama wa watumishi wa Kanisa na wengine hata kuuwawa. Mfano wa wazi ni wa kuuwawa Mchungaji wa Kanisa mojawapo huko Buselesele-Geita. Kifo chake ni matokeo ya wazi ya uchochezi unaotolewa kiwaziwazi kama alivyofanya mmoja wa mashehe wa huko Mwanza aliyesema wazi wazi kuwa ‘ukimuona Kadinali ua, ukimwona Askofu ua, ukimwona Mchungaji au Padri ua; iwe ni kwa wazi au kwa kificho. Tunashangaa kuona serikali haijamchukulia hatua kwa uchochezi huo. kwa hiyo tunatafsiri kuwa kifo cha Mchungaji wa Buselesele kuwa ni mwanzo tu wa vifo vya watumishi na wakristo wa Tanzania. Kwa hiyo tunaiomba serikali ielewe kuwa kifo cha Mkristo mmoja ni tangazo la kifo kwa wakristo wote.
2.    CCT inaikumbusha Serikali kwa mara nyingine kwamba nchi yetu inatawaliwa kwa kufuata misingi ya Katiba na Sheria inayobainisha kwamba Serikali haifungamani na dini yoyote. Na hakuna Kiongozi wa Serikali anayeweza kuisemea dini au Kiongozi wa dini anayeweza kuisemea Serikali. Kwa maana hiyo basi viongozi wa Serikali wasiwe na tabia ya kuegemea upande mmoja na kuulemea upande mwingine.
3.    Maadamu sasa imekuwa dhahiri kuwa kuchinja nyama itakayotumiwa na walaji wengi ni jambo la ibada linalogusa imani ya dini husika, kwa msingi huo huo na kwa mantiki hiyo hiyo watu wengine wa imani nyingine wasilazimishwe na kiongozi wa aina yoyote kushiriki jambo la kiimani na kiibada lisilowahusu.
4.    CCT inawatia moyo wakristo wasiopenda kushiriki mambo ya imani na ibada zingine zisizowahusu kwamba wasishurutishwe kushiriki imani na ibada hizo wasizohusika nazo kwa namna iwayo  yoyote ile.
5.    Aidha CCT kwa kuheshimu mchango wa Hayati Askofu Dkt. Laiser inawasihi Wakristo waendelee kutoa ushirikiano na vyombo vya dola na jamii vinavyotenda haki katika kudumisha amani, mshikamano, utulivu na umoja wa kitaifa.
Mungu ailaze pema roho ya Hayati Askofu Dkt. Thomas O. Laiser: BWANA ALITOA NA BWANA AMETWAA, JINA LA BWANA LIBARIKIWE.
Mungu Ibariki Afrika, Mungu Ibariki Tanzania.
BWANA AWABARIKI! AMEN.


« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment