Jumuiya ya Taasisi za Vyuo vya Elimu ya Juu Tanzania(TAHLISO) imewaonya wanaotumia kifo cha Mwanafunzi Akwilina Akwilini kisiasa huku wakitumia mwamvuli wa jumuiya hiyo kutoa matamko mbalimbali waache tabia hiyo vinginevyo watachukuliwa hatua.
Aidha, Jumuiya hiyo imewaomba wanafunzi kuendelea kuwa watulivu kusubiri matokeo ya uchunguzi wa kifo cha Akwilina na kujiepusha na maandamano na vitendo vyovyote vya uvunjifu wa amani.
Onyo hilo limetolewa leo mjini Dodoma na mwenyekiti wa jumuiya hiyo, George Mnali alipokuwa akizungumza na vyombo vya habari wakati wa kikao na kamati tendaji ya Tahliso kwa ajili ya kujadili changamoto zinazowakabili wanafunzi wa vyuo vikuu nchini.
Kikao hicho kimehusisha Marais wa serikali za wanafunzi wa Vyuo hivyo nchini, Mnali amesema Tahliso ndio chombo kikuu cha kuwasemea wanafunzi wote nchi nzima na sio kikundi kingine chochote.
“Vipo vikundi vingi vimejitokeza na kutoa matamko mbalimbali baada ya kifo hiki cha Mwanafunzi mwenzetu Akwilina Akwilini kutokea, vikundi vingine vikaenda mbali zaidi kwa kuwataka baadhi ya watendaji wa serikali akiwemo Waziri wa Mambo ya Ndani Kujiuzulu jambo ambalo linaashiria vikundi hivyo kutumika kisiasa,”amesema
Ameeleza kuwa haiwezekani kutaka watendaji wa serikali wajiuzulu wakati uchunguzi bado unafanyika na matokeo ya uchunguzi bado hayajatoka.
“Jambo la kusikitisha zaidi kuna baadhi ya vikundi vimejitangaza kwamba vinaungwa mkono na Marais wa Vyuo Vikuu jambo ambalo sio la kweli,”amesema Mwenyekiti huyo.
Ametoa wito kwa vikundi vyote vinavyojihusisha na kutumia mwamvuli wa Marais wa Vyuo Vikuu kama kinga yao ilikuuhadaa umma kwamba wanaungwa mkono, viache tabia hiyo vinginevyo watachukuliwa hatua.
No comments
Post a Comment