Writen by
sadataley
10:44 AM
-
0
Comments
Serikali ya Tanzania imewataka mabalozi wa kigeni wanaoziwakilisha nchi zao nchini humo, kutambua mazingira yanayolikabili taifa hilo kabla ya kutoa ripoti ambazo hazijathibitishwa na zenye uchochezi.
Hayo yamesemwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk Augustine Mahiga wakati akizungumza na vyombo vya habari jana jijini Dar es Salaam. Amesema kuwa, Tanzania kwa upande wake inakaribisha mazungumzo yenye uwazi kati yake na marafiki na katika masuala mbalimbali yanayohitaji ufafanuzi ili wawe na taarifa sahihi za mambo kuhusu yanayojiri nchini humo.
Mahiga ameongeza kwamba, vyombo vya usalama nchini Tanzania vimeendelea kufuatilia masuala magumu ya uchunguzi wa matukio yaliyojiri hivi karibuni yenye viashiria vinavyotishia usalama na amani na kuhusiana na masuala ya kisiasa nchini. Kauli hiyo imekuja ikiwa ni katika kujibu taarifa iliyotolewa siku chache zilizopita na balozi za Marekani, Umoja wa Ulaya (EU) na baadhi ya mataifa ya Magharibi nchini humo kuelezea shaka na wasi wasi wao kuhusiana na matukio ya kiusalama yaliyotokea hivi karibuni ndani ya taifa hilo mwanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki. Katika taarifa hiyo, balozi hizo zilisema kwamba matukio hayo ni tishio kwa demokrasia na utawala bora kwa nchi kama Tanzania.
Akijibu taarifa hiyo Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk Augustine Mahiga amesema kwamba taarifa zilizotolewa na nchi hizo zinaonyesha ni kwa kiasi gani balozi hizo zisivyofahamu changamoto za kiusalama na kisiasa zinazolikabili taifa hilo tangu miezi 18 iliyopita. Dk Mahiga ambaye ameshawahi kuiwakilisha Tanzania kama balozi wa kudumu wa nchi hiyo katika Umoja wa Mataifa, amesema kwamba ni kawaida kwa mabalozi wa kigeni kufuatilia masuala ya kisiasa na kiusalama katika nchi walizopo na kupeleka taarifa katika nchi zao.
Parstoday
No comments
Post a Comment