Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Saturday, October 28, 2023

 

KKKT- DMP USHARIKAA WA KIJITONYAMA

SIKU YA BWANA YA KUKUMBUKA MATENGENEZO YA KANISA (Reformation)

USHUHUDA WETU- TUNATENGENEZA MAMBO YALIYOHARIBIKA

ZABURI 25:14-22, 1KOR  3:16-17, YOHANA 2:15-17

29.10.2023

 

Leo tunatafakari juu ya matengenezo ya Kanisa ambayo ndio ushuhuda wetu. Ushuhuda ni neno la kuthibitisha na kuelezea mambo yalivyokuwa au kutokea, ni uthibitisho/ushahidi.

 

Mungu alipoumba dunia na kuifanya kuwa kanisa lake halikuwa na haja ya matenegenezo kwa sababu aliona kila kitu ni chema (Mw 1:31) Ila baada ya anguko ndipo umuhi wa matengenezo ulipoanza kuonekana.

 

Matengeno ya Kanisa yalianza mara moja baada ya anguko la mwanadamu, mwanadamu alianza kuona udhaifu na Mugu akaona mtu wake anahitaji matengenezo ili aweze kuwa mwema tena ndipo Mungu aliamua kuanza matengenezo kwa kuwatengenezea Mavazi ya ngozi wanadamu wale wa kwanza kuficha udhaifu. (Mwanzo 3:21)

 

Tunamuona pia Yoshua alipoona Kanisa la Mungu linataka kujichanganya na miungu mingine aliamua kusimama na kuonyesha msimamo kuwa Kanisa lenye michanagnyiko linahitaji kutengenezwa na liwe na msimamo mmoja ndipo aliposema mimi na nyumba yangu tutamtumikia Mungu kama ninyi mnataka kuendelea kuabudu miungu. (Yoshua 24:15)

 

Katika Agano Jipya kwanza tunamuona Yesu mwenyewe katika somo tulilolisoma alipofika Yerusalemu na kukuta hekaluni zinafanyika biashara na sasa kugeuzwa kuwa soko aliamua kufanya matengenezo yake kwa  kuondoa uchafu wote na wafanya biashara wote kule hekaluni. (Yn 2:13-17)

 

Tunamuona Mtume Paulo nae anaweka mkazo zaidi kwa kuwataka Wakoritho kujitambua zaidi kwamba wao  ni hekalu la Roho Mtakatifu. Kutokukubaliana na mambo ya hovyo hovyo yafanyike na wao kukaa kimya. hata sasa wengi tumekaa kimya na tunashindwa  kukemea na kuingia na kufanya matengenezo huku tukishuhudia utapeli na ongezeko la waalimu wa uongo linazidi ndani ya Kanisa ambalo Mungu amelinunua kwa bei ya thamani.

 

Matengenezo ya Kanisa yaliendelea baadae na hata kuzaliwa kwa Kanisa la Kilutheri Duniani,  sasa katika somo hili nataka ujiulize kwa nini wewe ni Mlutheri? na Mlutheri ni nani?

 

Yawezekana usiwe na majibu ya haraka ila nitakapofikia mwisho wa somo hili utapata majibu.

 

Kanisa letu la Kilutheri kila Jumapili ya kila mwaka mwishoni mwa mwezi wa kumi karibu na tarehe 31 huadhimisha sikukuu ya matengenezo ya kanisa yaliyofanyika tarehe 31/10/1517.

Ilipofika mwakani (2017) Kanisa la kilutheri Duniani lilifikisha miaka miatano(500) ya matengenezo yake, Lazima tujihoji je bado tupo kwenye msingi wa neno la Mungu au tayari tumeshatoka? Tufanye nini ili kuendeleza kazi njema ya Kuutangaza ufalme wa Mungu hapa duniani? Matengenezo haya lazima yawe ushuhuda wetu kweli katika matendo yetu na sio kinadharia tu.

 

USHUHUDA WETU

Kama nilivyoeleza maana ya Ushuhuda wetu mimi nina ujasiri wa kusema kuwa nimekuwa Mlutheri kwa sababu nilizaliwa katika imani hiyo nikiendelea kujiboresha kumjua Mungu zaidi.

 

Jina mlutheri limetokana na chimbuko toka jina la Dkt. Martin Luther, baba wa matenegenezo ya kanisa aliyekuwa na lengo la kurekebisha na kutengeneza baadhi ya mafundisho na taratibu zilizokuwa zikifanywa na kanisa la wakati ule kanisa la Kirumi(RC) ambazo zilikuwa hazijengwi kweneye msingi wa Neno la Mungu ili kurejea katika msingi wa Kibiblia.

 

Dkt. Martin Luther alizaliwa na kukulia nchini Ujerumani na alisoma masomo ya falsafa na sheria akiwa kijana mdogo, lakini baadae aliamua kujiunga na masomo ya Theolojia ambapo mwaka 1507 alibarikiwa kuwa padre wa katoliki na baadae alifundisha chuo cha theolojia Wittenberg. Wakati akifundisha chuoni Luher alichukizwa na mafundisho na matendo yaliyokuwa yakifanywa na Kanisa katoliki kama vile mamlaka ya papa, vyeti vya msamaha, wakristo kuzuiwa kusoma biblia nk, ndipo tar 31/10/1517 aliandika maoni (sentensi) 95 kwenye mlango wa Kanisa la Wittenberg  ambazo zilizungumzia juu ya ukosefu wa elimu ya Kibiblia, matendo mabaya na kutokuwajibika miongoni mwa viongozi wa Kanisa, yeye alikuwa na lengo la kuwarejesha kwenye maandiko Matakatifu.

 

Dr martin Luther alisimamia ukweli wa neno la Mungu katika kupambana na mafundisho potofu yaliyofanya wokovu ufikie hatua ya kununuliwa kwa hela kupitia vyeti vya msamaha pamoja na mapungufu mengine. Tunaweza kusema kuwa Luther alishuhudia ukweli wa injili kiasi cha kuwa tayari kufa kwa ajili ya ukweli pale aliposema “Hapa nasimamia ukweli wa neno la Mungu, sitabadili msimamo, nisaidie Mungu wangu” “Here I Stand, Lord Help Me”

 

Dkt. Martin Luther hakuwa na lengo wala nia ya kuanzisha dhehebu jipya, bali alitaka tu kusahihisha kile alichokiona kama ukiukwaji wa wazi wa mafundisho ya Biblia ila alitakiwa kukana maandishi yake ila alisema asipothibitishiwa kutoka biblia kuwa amekosea hayupo tayari kuyakanusha ndipo alipohesabiwa kuwa mzushi na kuhukumiwa Kunyongwa ila alifanikiwa kutoroka na kujificha.

 

Ndipo mwaka 1597 watheolojia waliokaa katika mji wa Wittenberg huko ujerumani walitafsiri jina ulutheri kumaanisha ‘Kanisa la kweli’ ambalo limejengwa kweneye msingi wa neno la Mungu ila Martin Luther alipendelea neno Kiinjili zaidi.

 

Hivyo tunaitwa Walutheri kwa sababu tunafuata misingi na mafundisho ya Dr. Martin Luther na aliweka mkazo katika mambo haya: -

  1. Mafundisho rasmi ya Kilutheri ya wakati wote na mahali pote huonyesha sisi sote

wenye dhambi na tunapokewa jinsi tulivyo kwa neema ya Mungu lakini hatuaswi kubaki jinsi tulivyopokelewa.(Rumi 6:1-4) na tujue kuwa ya kale yamepita tutazame mapya (1Kor 5:17) na tukazane kuzaa matunda(Mt 7:19) na huku tukiwajali wengine (Mt 25:36-46).

  1. Leo hii Mlutheri anafahamika kuwa ni muumini wa dini ya Kikristo ambaye

anaabudu katika Kanisa la Kiinjili la Kilutheri ambalo ni ushirika wa watakatifu ambao injili inatangazwa kwa usafi na sakramenti zinatolewa kwa usahihi wake. Kama Luther alivyotafsiri maana ya Kanisa kuwa ni pale ambapo injili inahubiriwa na kupokelewa tena na Sakrament ya Ubatizo na Ushirika wa Meza ya Bwana vinatolewa kwa usahihi wake.

  1. Mlutheri anamwamini Yesu Kristo kuwa Bwana na Mwokozi wa maisha yake na

kubatizwa katika Utatu Mtakatifu, ambapo anasafishwa dhambi zake na kupokelewa katika kundi la waaminio na kufanyika mwana wa Mungu  kwa njia ya imani tu. (SOLAR FIDES)- Roman 1:17.

  1. Mlutheri anaamini juu ya mafundisho, mafunuo, mapenzi na ahadi za Mungu

kupitia maandiko matakatifu yaani Biblia, kuwa ndio msingi wa maisha yake. (SOLAR SCRIPTURA).

  1. Mlutheri anakubali na kuamini ya kuwa wokovu wa mwanadamu unapatikana

kwa Neema ya Mungu tu. (SOLAR GRATIA).

  1. Mlutheri anakubali na kuamini ya kuwa katekisimo ndogo ya Dkt Martin Luther,

ukiri wa Nikea, Mitume, Athanasio na ungamo la Augusburg lisilobadiika ndio maelezo sahihi tena ya wazi ya neno la Mungu

 

KKKT imejali maisha wa kiroho ya waumini wake kwa kuzingatia Biblia na kuna vitabu vingine kama kitabu cha nyimbo TUMWABUDU MUNGU WETU pamoja na kalenda ya mwaka inayomwongoza kila mlutheri popote alipo kwa neno la Mungu kila siku asubuhi na jioni.

 

Nyakati hizi kumetokea mafundisho mengi sana ambayo yanawachanganya washarika wetu. Ni lazima sisi tufuate na kuenzi utaratibu wa ibada yetu ili watu waweze kutambua kuwa sisi walutheri wenye umoja na tumebobea katika mafundisho sahihi ya neno la Mungu na sakramenti zake zinatolewa kwa usafi wote

 

Kwa msingi wa katiba ya KKKT tunapaswa kuuenzi, kuulinda na kuimarisha umoja wetu, twapaswa sisi kushuhudia kila kona juu ya neema ya Mungu kwetu. Waasisi wa KKKT waliweka wazi msingi wa Imani utakaofuatwa  ambao ni

 

 Kanisa lililojengwa juu ya msingi mmoja, Yesu Kristo, hukiri kwamba Neno la Mungu lililoandikwa katika Agano la Kale na Agano jipya  ndio msingi pekee wa uhakika wa Imani na maisha ya kanisa. Katika umoja wa Kanisa moja duniani, huungama ungamo la Mitume, Nikea, na la Athanasio; hukubali pia maungamo ya Kanisa la Kilutheri hasa ungamo la Augusburg lisilobadilishwa na katekisimo ndogo ya Martin Luther kuwa maelezo au mafafanuzi sahihi ya neno la Mungu. Sharika zote, na wachungaji, sinodi na dayosisi za kanisa hili zitakubali na kufuata nsingi huu wa imani.

 

HITIMISHO

Tunapoona habari hizi za matengenezo ya kanisa na historia nzuri za watu waliotetea imani yao hata kwa mateso yatatuhimiza sisi wa leo kuendelea kuona kuwa kanisa la Mungu linapaswa kujifunza kwa usahihi ukweli wa neno la Mungu pasipo kuyubishwa.

 

Tunapoona neno la Mungu linayumbishwa tusikubali hali hiyo tunapaswa kukemea kwa ukali kama alivyofanya katika hekalu ya Yerusalemu na tunapaswa kupatwa na wivu tunapoona kweli ya neno la Mungu inapindishwa.

 

Matengenezo ya Kanisa ni jambo endelevu ili kuendelea kupokea neema ya Mungu katika ukombozi kwenye maisha yetu.

 

Tunapewa pia wito wa kujenga umoja wetu katika familia zetu, umoja wa kifamilia, umoja wa jumuiya na sala, umoja wamitaa ya Sharika, umoja wa sharika, umoja wa jimbo, Dayosisi na Kanisa zima.

 

Wapendwa washarika kwa kupitia siku hii ya matengenezo ya kanisa, tunaletewa wito kujifanyia tathimini katika Imani zetu, mienendo na maisha yetu kwa ujumla. Je bado tupo katika msatari wa kumfuata Yesu au la? Lazima tujihoji je bado tupo kwenye msingi wa neno la Mungu au tayari tumeshatoka? Tufanye nini ili kuendeleza kazi njema ya Kuutangaza ufalme wa Mungu hapa duniani? Matengenezo haya lazima yawe ushuhuda wetu kweli katika matendo yetu na sio kinadharia tu.

 

Mungu na atusaidie sote, amen.

NEXT »

No comments

Post a Comment