Writen by
sadataley
5:53 PM
-
0
Comments
Dar es Salaam. Baada ya makada kumaliza kurejesha fomu za kuomba kugombea urais kwa tiketi ya CCM jana, macho sasa yanaelekezwa kwenye vikao vya juu vya chama hicho vitakavyotoa majina yasiyozidi matano yatakayokwenda kupigiwa kura na Mkutano Mkuu utakaofanyika Julai 11 na 12.
CCM imeshatangaza kuwa itatumia vigezo 13 ilivyojiwekea kuwachambua wagombea 41 waliochukua na kurejesha fomu ili kupata majina ya wachache watakaopigiwa kura na mkutano huo mkuu, lakini Kamati ya Wazee, ambayo itatoa ushauri utakaokuwa msingi wa uamuzi wa vikao vingine na Kamati Kuu, italazimika kuangalia sifa za ziada katika kuchuja watangazania hao.
Kamati ya Wazee, inayohusisha wenyeviti na makamu wao wa zamani wa CCM pamoja na marais wa zamani wa Zanzibar, imeripotiwa kuanza kazi ya uchambuzi na itawasilisha taarifa yake kwa Kamati Kuu itakayokutana Julai 9 na baadaye kupeleka mapendekezo yake kwenye Halmashauri Kuu, ambayo huandaa ajenda za Mkutano Mkuu.
Wakati vikao hivyo vikiandaliwa, uzoefu unaonyesha kuwa CCM huzingatia mambo mengi katika kufanya uchambuzi, ikiwa ni pamoja na uteuzi wa mtu atakayeondoa makundi yaliyoundwa wakati wa kuelekea uteuzi wa mgombea urais wake, kuzingatia Muungano, jinsia, eneo la kijiografia, rekodi ya mtiania, mustakabali wa uongozi wa chama na kukubalika kwa kada, hasa katika kipindi hiki ambacho upinzani umeongezeka nguvu.
“Kuna katiba za aina mbili,” alisema mmoja wa makada ambaye aliomba jina lake lisitiriwe. “Katiba ya maandishi ambayo inatoa mwongozo wa kisheria wa namna ya kumpata Rais wa nchi, lakini pia kuna katiba ya kimtazamo ambayo si rasmi, bali ni fikra za watu wanapozungumzia aina ya rais wanayemfikiria.
“Mfano, kama kuna eneo fulani halijawahi kutoa kiongozi wa nchi, kipindi hiki sasa ni chao.”
Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa na Mwananchi uliojumuisha mahojiano na baadhi ya makada wenye uzoefu na mchakato wa uchaguzi ndani ya CCM, mgombea wa chama hicho tawala anaweza kutoka katika makundi manne ambayo gazeti hilo limeyaita kundi la kifo, kundi la mteule mbadala, kundi la vijana na wanawake.
Iwapo mteule hataweza kutoka kwenye kundi la kifo, ambalo linajumuisha makada wenye nafasi kubwa ya kupitishwa, chama hicho kinaweza kuamua kuchukua mwanachama ambaye atatoka kundi la wateule mbadala kwa lengo la kuzika makundi makubwa yaliyozuka wakati huu, au kuteua kada kijana iwapo CCM itakuwa inataka mwelekeo mpya, au mgombea mwanamke kama ilivyokuwa mwaka 2010 ilipoamua kuachana ghafla na Samuel Sitta na kumweka mbele Anne Makinda kuwa Spika wa Bunge, kwa maelezo kuwa umefika wakati wa wanawake.
Kundi la kifo
Kwa mujibu wa wachambuzi hao, kundi la kifo linaweza kuwa na makada sita ambao ni Profesa Mark Mwandosya, Steven Wasira, Frederick Sumaye, Edward Lowassa, Bernard Membe na Mizengo Pinda.
Katika kundi hilo, Mwandosya amekuwa hahusishwi na kashfa wala kuwa na migogoro na makada wengine. Aligombea kwa mara ya kwanza mwaka 2005 na kushika nafasi ya tatu, akiwa nyuma ya Jakaya Kikwete, aliyeshinda na Dk Salim Ahmed Salim.
Pamoja na kutokuwa na mivutano na watu, Profesa amekuwa hasikiki kutokana na kupewa kazi inayomweka mbali na wananchi.
“Kuendelea kuwamo ndani ya Serikali hadi sasa, katika macho ya wengi, ataonekana hana jipya,” alisema mchambuzi huyo akimzungumzia Profesa Mwandosya ambaye ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu).
Kundi hilo pia linamjumuisha Wasira ambaye uzoefu wake mkubwa ndani ya chama na Serikali unampa nafasi kubwa ya kupewa dhamana hiyo. Amekuwa akitumiwa na CCM kutetea utendaji wa Serikali na hivi sasa amepewa jukumu la kuongoza kamati inayoandaa Ilani ya Uchaguzi.
Ukweli ni kwamba anatoka Kanda ya Ziwa, ambayo kichama ni kubwa kwa maana ya idadi ya wajumbe wa Mkutano Mkuu, jambo linalompa nafasi kubwa ya kushinda iwapo jina lake litakwenda kwenye chombo hicho cha mwisho cha uamuzi.
Lakini nafasi yake inakuwa finyu kutokana na wakosoaji kumwona kuwa amepoteza mvuto baada ya kufanya kazi kwenye Serikali za awamu zote nne bila ya kuwa na kitu kinachomtofautisha na wengine na hilo linaweza kuipa nguvu Kamati Kuu kumwengua.
Pia, wamo mawaziri wakuu wa zamani, Frederick Sumaye na Edward Lowassa ambao wote walishawahi kuingia bila mafanikio kwenye mbio za urais kwa tiketi ya CCM.
Sumaye, ambaye alikuwa Waziri Mkuu kwa miaka 10 mfululizo katika Serikali ya Awamu ya Tatu, aligombea mwaka 2005 lakini jina lake lilikatwa. Ni mtu ambaye hana makundi kwenye chama, amepangua tuhuma dhidi yake na daima amekuwa akionyesha wazi chuki yake dhidi ya rushwa.
Baada ya mawaziri wakuu kugonga mwamba katika chaguzi zilizopita, safari hii Sumaye atakuwa akitegemea kuwa, kati ya watatu walio kwenye kinyang’anyiro hicho, atapitishwa.
Lakini uzoefu wake kwenye nafasi ya waziri mkuu kwa kipindi chote cha miaka 10 na chuki yake ya wazi dhidi ya rushwa, hakuwezi kuwa sifa pekee. Bado hajajiimarisha ipasavyo ndani ya chama, ambacho kwa kumteua mgombea urais, kitakuwa kimempata mwenyekiti wake wa miaka 10 ijayo.
Atalazimika kushinda ushawishi wa wapinzani wake waliowahi kushika nafasi hiyo, Lowassa na Pinda ili apitishwe na CCM.
Kamati Kuu itakuwa na kazi ngumu itakapokutana na jina la Lowassa, Mbunge wa Monduli ambaye alikuwa amekaa kimya kwa muda mrefu tangu alipojiuzulu uwaziri mkuu mwaka 2008 kutokana na sakata la Richmond, lakini amerejea kwa kishindo katika miaka miwili iliyopita.
Lowassa amejijenga ndani ya CCM na ameonyesha nguvu yake ya kuungwa mkono na wanachama na watu wengine walio nje na pia wakati alipotangaza nia na baadaye kuzunguka mikoani kusaka wadhamini.
Kauli ya Rais Kikwete kuwa CCM inataka mtu ambaye anaungwa mkono ndani na nje ya chama imeitia nguvu kambi yake na amekuwa akitumia kauli ya Baba wa Taifa Mwalimu Julius Nyerere ya chama hicho kuongoza mabadiliko, akijinadi kuwa ndiye anayeweza kuongoza mabadiliko hayo.
Chanzo: mwananchi.co.tz
Subscribe to:
Post Comments
(
Atom
)
No comments
Post a Comment