Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Saturday, March 29, 2014

Kanisa lafunga kuombea Bunge la Katiba

“Kwa hali ilivyo sasa bungeni, tusitegemee kupata Katiba au ikipatikana inaweza kutokidhi matakwa ya wananchi kwa sababu tayari wanaoitengeneza wamegawanywa. Tunamwomba Mungu aingilie kati.” Lucas Mwakalonge 
Na Editha Majura, Mwananchi
Dodoma. Kanisa la Makole Pentekoste Holyness la mjini hapa, linafanya maombi maalumu ya kuliombea Bunge Maalumu la Katiba baada ya kutoridhishwa na mwenendo wa Bunge hilo.
Maombi hayo yaliyoanza Jumatatu, yanatarajiwa kumalizika Jumapili ijayo kwa waumini kugawanyika makundi, kila moja linaomba kwa kufunga kwa siku moja kabla ya kujumuika pamoja kanisani, Jumapili kuomba kwa pamoja.
“Kificho (aliyekuwa mwenyekiti wa muda wa Bunge hilo) aliliongoza bila kanuni ingawa kulikuwa na mvutano haukuwa mkubwa na alipochaguliwa Sitta kuwa mwenyekiti wa kudumu wananchi wengi tulifurahi,” Mchungaji Kiongozi Asajile Mwandiga alisema na kuongeza.
“Kwa tulivyomfahamu uwezo wake wa kuongoza, kwa mfano Bunge la Tanzania la 9, tuliamini tungepata Katiba bora lakini imekuwa kinyume, anaegemea upande wa chama chake kwa uwazi kabisa.”
Mch. Mwandiga alisema hali hiyo iliwakatisha tamaa, lakini kwa kuwa wanaamini katika Mungu, sasa wanaongoza Kanisa kuomba msaada wake ili abadilishe mioyo ya wanaopindisha mambo.
Naye Mchungaji kiongozi msaidizi wa kanisa hilo, Lucas Mwakalonge, alisema tofauti na Bunge kuamua mambo kwa mtindo wa wengi wape, wao wanaoamini katika Mungu.
Mwakalonge alitaja sababu nyingine za maombi hayo kuwa ni mivutano ya mara kwa mara bungeni kiasi cha vikao kuvunjika na mgawanyiko wa Wabunge wa Bunge Maalumu.
Mchungaji huyo aliyekuwa Mkurugenzi Msaidizi wa Idara ya Maktaba na Tafiti ya Bunge la Jamhuri ya Muungano hadi alipostaafu mwaka 2011, alisema ili kufikia uamuzi wa kutoa Katiba bora ni lazima kuwe na umoja miongoni mwa wanaoiunda na kuiandika.
“Kwa hali ilivyo sasa bungeni, tusitegemee kupata Katiba au ikipatikana inaweza kutokidhi matakwa ya wananchi kwa sababu tayari wanaoitengeneza wamegawanywa. Tunamuomba Mungu aingilie kati,” alieleza.
Mbali na hayo, Mwakalonge alisema wanataka uwezo wa Mungu uzuie mambo yasiyompendeza kuingizwa kwenye Katiba, akitoa mfano wa sura ya 4 inayohusu Haki za Binadamu, kwamba kusiwe na utetezi wa mashoga na wasagaji.
“Kuna mambo hakika hayapaswi kuingizwa kwenye katiba yetu, tunamuomba Mungu apitishie mbali wale wote wanaotaka kuifanya katiba hii kama mchezo wa kuigiza,” alisema
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment