Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Monday, May 13, 2013


ASKOFU WA  KANISA LA KIINJILI LA KILUTHERI TANZANIA  DAYOSISI YA IRINGA
DKT.O.M MDEGELLA
AZINDUZI WA USHARIKA WA NYAMHANGA
JIMBO  LA  KUSINI  MAGHARIBI(IHEMI)

1. HISTORIA  YA  USHARIKA  WA  NYAMHANGA.

Bwana  Yesu  Asifiwe.

Tunawasalimu  katika  jina  la  Mwokozi  wetu  Yesu  Kristo.

Nyamhanga ilikuwa moja kati ya Mitaa kumi na mbili (12) ya Usharika wa Ipogolo.

Msukumo wa kuanzishwa mtaa wa Nyamhanga ulitokana na mara kwa mara Washarika kukosa huduma za kiroho hasa nyakati za mvua nyingi  ilikuwa vigumu kwa wazee, wagonjwa na watoto kuvuka korongo lililopo kati ya Usharika wa Ipogolo na eneo la  Nyamhanga.

Mwanga ulianza kujitokeza pale mzee wa kanisa Dauson Mbembe alipombatiza ubatizo wa dharura mgonjwa mahututi ndugu Yohana Mnyihanga  tarehe 12/10/1992.

Wakati huo Usharika ulikuwa unaongozwa na Mwinjilisti Yona Kinganga (Kaimu Mchungaji) baada ya Mchg Sawike kuhama.
Kutokana na tukio hilo kaimu Mchungaji alimwomba aliyebatizwa (ndg. Yohana Myihana) nyumba yake itumike kwa sala za asubuhi, alikubali na huduma hiyo ilikaanza  tarehe 15/10/1992.
Huduma zingine ziliendelea kutolewa Usharikani Ipogolo.

Kaimu Mchungaji alipoona maendeleo ya  sala za asubuhi zinaendelea vizuri, aliwaruhusu Washarika waliokuwa wakiishi eneo la Nyamhanga kuanza maandalizi ya kuanzisha mtaa ili huduma za kiroho ziweze kufanyika katika eneo hilo.

Mnamo  mwaka 1993  sala za asubuhi zilihamia nyumbani kwa mzee Mbwilo (Baba Tula ) kukiwa na washarika wanane (08) chini ya uongozi wa mzee wa kanisa Ndugu Dauson  Mbembe.

Uongozi wa maandalizi ya Mtaa huo ulibuni mbinu mbalimbali za kuanzisha Mtaa  ikiwa ni  pamoja  na:-
-          Kuanzishwa kwaya  ya  Upendo ambayo  inaendelea  na  uimbaji  hadi  sasa.
-          Kuwa  na  minada  ya  aina  mbalimbali.
-          Kuanzisha Uinjilisti wa nyumba  kwa nyumba siku za Jumanne na Mikesha ya mara kwa mara.
-          Kuundwa  kwa  kamati  ya majengo.

Kwa  kutumia  mbinu  tajwa  hapo juu tarehe 13/8/1993  tulifanikiwa kununua  kiwanja  chenye ukubwa wa robo tatu eka (3/4) toka  kwa  mzee  Pauli  Kanuru  kwa Tsh  elfu tatu (3,000).Hatua hii  ya  kupata kiwanja iliwasukuma washarika kuanza kukusanya mawe kwa ajili ya  ujenzi  wa  kanisa.
Kiwanja hicho kipo mwambao wa daraja la Cagrielo, hakijapimwa na  kinatumika kama  shamba la viongozi wa kanisa.

Mnamo mwaka 1994  chini ya Mwenyekiti wa majengo Ndugu Awarywa Nnko tulipata kiwanja kilichopimwa.
Kutokana na kupatikana kwa kiwanja hicho uongozi uliamua kanisa  lijengwe katika kiwanja hicho, ndipo washarika walipoanza shughuli za ufyatuaji wa matofali. Tunamshukuru  Mungu kwa kuwatumia watumishi wake Ndugu Awarywa Nnko na Ndugu Chua kusimamia usombaji wa kuni za kuchomea matofali kwa trekta lililotolewa na Shirika la kilimo (EEC).

Trekta hili lilitumiwa pia kipindi hicho kusomba  matofali  ya  awamu  ya  kwanza. Kazi ya ufyatuaji na uchomaji wa matofali ya awamu ya pili zilifanyika mnamo mwaka 1995. Kutokana na mzee Mbwilo kuhamia Makete  sala za asubuhi zilihamishiwa nyumbani  kwa  mzee  Dauson  Mbembe  kuanzia  tarehe  14/7/1995.

Katika kipindi hiki Uongozi uliomba huduma ya shule ya Jumapili (Sunday  School) ianze, uongozi wa Usharika ulikubali na watoto walianza ibada za Shule ya Jumapili tarehe 19/10/1996.
Kazi ya ujenzi wa kanisa ilianza rasmi tarehe 26/9/1996.
Ili kufanikisha ujenzi wa kanisa zilibuniwa mbinu au njia mbalimbali zikiwemo:-
-          Kuanzisha mgahawa.
-          Bahati na sibu iliyotupatia Tsh laki mbili na elfu hamsini (250,000)
-          Wahisani R.C Ipogolo walitupatia Tsh elfu ishirini (20,000).
-          Harambee iliyoongozwa na Mchg Agness Kulanga ilitupatia Tsh laki moja elfu thelathini  (130,000).
-          Makanisa rafiki wa Usharika wa Ipogolo toka Augustana Marekani walitupatia bati sitini (60) gage 28.

Kutokana na Ndugu Awarywa Nnko kupata uhamisho wa kikazi mwaka 1997, Ndugu Mathew Mlangi alichaguliwa kushika nafasi ya Mwenyekiti wa Majengo.
Ndugu Mathew Mlangi  alisimamia kamati hiyo ya Majengo, awamu ya pili ya usombaji wa tofali kwa ajili ya ujenzi wa kanisa.

Ndugu Mathew Mlangi alienda masomoni nje ya nchi, na ndg Henry Mwaipopo alichaguliwa kuchukua nafasi ya uwenyekiti wa majengo, Ili kuharakisha ujenzi wa kanisa unaendelea bila kukwama.
Wakati ujenzi wa Kanisa unaendelea, Uongozi  uliamua, ibada za shule ya Jumapili pamoja na mazoezi ya uimbaji yafanyike kwenye jengo la kanisa lililokuwa linaendelea kujengwa (pagale).

Uongozi wa Mtaa wakati huo ulipata changa moto nyingi kutoka kwa wamiliki wa kiwanja cha kanisa. Kanisa lililazimika kulipa fidia ya Tsh elfu ishirini na tano (25,000) kwa wamiliki wa eneo hilo kwa ajili ya vitindi na mlimao kama ilivyoamuliwa  na  ofisi  ya  Kata ya Kitwiru.

Tunamshukuru sana Mungu kupitia kwa msaidizi wa Askofu wakati huo Mchg Dr Richard Lubava na aliyekuwa Mchg wa Usharika wa Ipogolo Mchg Lusungu Msigwa waliweza kuishawishi ofisi ya bega kwa bega ambayo ilitupatia Tsh Milioni tatu laki nne elfu kumi tatu na mia nne (3,413,400), saruji mifuko mia moja (100), mbao mia moja (100), chokaa mifuko miwili (02) na waya za “Ringbeam”.

Mchango huu pamoja na michango ya washarika ilifanikisha kazi ya ujenzi wa kanisa kukamilika kuta, kupaua na kuchonga  milango.
Shughuli hizi zilifanyika chini ya usimamizi wa mwenyekiti wa majengo Ndugu Henry Mwaipopo na mzee wa kanisa ndugu Dauson Mbembe.
 Kutokana na kukamilika kwa ujenzi wa kanisa tarehe 11/8/2002 ibada zote zilianza kufanyika yamhanga na ukawa mtaa unaojitegemea chini ya uongozi wa mzee wa kanisa Ndugu Dauson Mbembe, kukiwa na waumini sabini na mbili (72).

Huduma ziliendelea chini ya mzee wa kanisa Ndugu Dauson Mbembe  hadi tarehe 30/11/2002 Mtaa ulipopata mwinjilisti, Regina Kibasa. Mtaa ulipopata mwinjilisti, washarika walipata hamasa, na mikakati ya maandalizi ya kuchonga mabenchi, kutengeneza samani za ofisi, kuingiza umeme na maji zilianza.
Michango ya washarika wa Mtaa huu,  pamoja  na  minada  ya  ndani  kazi zote  hizo zilikamilika.
Baada ya Mtaa kukamilisha kazi zilizotajwa hapo juu, lilijitokeza wazo la kujenga nyumba ya mtumishi.

Washarika wa Mtaa huu, kwa michango yao na nguvu kazi wakishirikiana na vijana ishirini na moja (21) toka Usharika wa  Augustana  Marekani walifanikiwa kukamilisha kazi ya kujenga Msingi wa nyumba ya mtumishi.

 Mnamo mwaka 2004, uongozi wa Mtaa uliandaa harambee, na Baba Askofu DKT Owdenburg Moses Mdegella ukiwa mgeni rasmi katika harambee hiyo kwa lengo la kuhamasisha.
Waalikwa wengine walikuwa, Kwaya kuu toka Usharika wa Kanisa Kuu, viongozi  wa kanisa pamoja na viongozi wa Serikali, ndugu na marafiki.
Harambee hii ilichangisha kiasi cha Tsh  laki nane themanini na mbili elfu na mia tatu (882,300/=). Kiasi kilichopatikana katika harambee hiyo  kiliwezesha kukamilisha kazi ya ujenzi wa kuta, kupaua, Milango, kupiga plasta ndani.

Kazi hii ya ujenzi ilifanyika chini ya uongozi wa Mwilisti wa mtaa Regina Kibasa, wachungaji wa Usharika wa Ipogolo, Mchg Abass Tagamtwa na Mchg Nixon Mwitula.
Jengo la kanisa pamoja na nyumba ya mtumishi zilizinduliwa rasmi na Baba Askofu DKT Owdenburg Moses Mdegella tarehe 21/06/2009.

Mtaa wa Nyamhanga hadi kupata hadhi ya  kuwa Usharika umeongozwa na watumishi hawa wafuatao:-
1.     Mzee wa kanisa Dauson Mbembe           11/08/2012 – 30/11/2011
2.     Mwinjilisti Regina Kibasa                                     30/12/2002 – 30/11/2009
3.     Shemasi Regina Kibasa                             01/11/2009 – 14/12/2009 
4.     Shemasi Gaitan Mkemwa             15/12/2009 – 20/09/2011
5.     Mwinjilisti Aneth Mkongwa                      2009 – Hadi sasa ni Mwinjilisti wa
                                                                        Mtaa wa  Stesheni
6.     Mchg Nuru Makweta  -20/9/2011 hadi sasa ni Mchg kiongozi wa Usharika huu mpya.

Makatibu waliotumika hadi kupata Usharika ni hawa wafuatao:-
1.     Vicky Motto -                       2002
2.      Mathias .B. Masele –      2002 - 2006
3.     Noel Chengula  -                2006-Hadi sasa ni Katibu/Mtunza Hazina wa Usharika.

Tunamshukuru Mungu kwa kufanikisha upatikanaji wa  viwanja vinavyoungana na eneo la kanisa.  Viwanja hivi vilipatikana baada ya kanisa kulipa fidia ya Tsh Milioni saba laki moja na nne elfu mia tisa hamsini  (7,104,950/=) kwa waliokuwa wamiliki wa viwanja hivyo tarehe 04/02/2012.

Tunawapongeza  Wazee  wa  kanisa, Kamati ya majengo,Kamati ya ununuzi wa viwanja pamoja na wote  walioshiriki katika kufanikisha upatikanaji wa viwanja hivyo.


Imeandaliwa  na: KAMATI YA MAANDALIZI YA UFUNGUZI WA USHARIKA WA
                                NYAMHANGA:

Tarehe: 12/05/2013


2. RISALA

Baba Askofu wa Dayosisi ya Iringa. Msaidizi wa Askofu. Katibu Mkuu, Wakuu wa Majimbo, Wachungaji Wote, Viongozi wa Serikari na Waumini wote mliohudhuria katika ibada hii,
“ BWANA YESU ASIFIWE”

Baba Askofu.
Kwa niaba ya Washarika wa Usharika Mpya wa Nyamhanga, ambao baada ya muda mfupi ujao utaufungua, awali ya yote napenda kutoa shukurani zangu za dhati, kwanza kwako wewe Baba Askofu, Msaidizi wa Askofu, Katibu Mkuu, Wakuu wa majimbo, Viongozi wa Serikali na wote mliohudhuria katika ibada hii, kwa kumshukuru Mungu kutufikisha  siku ya leo.

Pia napenda kutoa shukurani zangu za dhati kwa Washarika wote wa Usharika wa Ipogolo na Wachungaji wote waliohudumu katika Usharika huo kwa kuuongoza Mtaa wa Nyamhanga hadi kufikia kuwa Usharika, na leo Baba Askofu utaufungua rasmi.
Ningependa Kuwataja  Wachungaji waliohudumu katika Usharika wa Ipogolo, Nyamhanga ukiwa moja wa Mitaa ya Usharika huo. Wachungaji hao ni hawa wafuatao:-

(1)  Mchungaji Agness Kulanga na msaidizi wake Mchg. Aleki Mhanga
(2)  Mchungaji Damian Ngandango
(3)  Mchungaji Lusungu Msigwa
(4)  Mchungaji Abbas Tagamtwa
(5)  Mchungaji Nixon Mwitula (Mchungaji Kiongozi wa Usharika wa Ipogolo hadi sasa) na wasaidizi wake wafuatao;- Mchg. Lunyiliko Muhile, Shemasi Gaitan Mkemwa, Mchg. Lucrecia Mbwilo, na Mchg. Nuru Makweta.
Wote hawa wamefanya kazi kubwa katika kuufikisha Mtaa wa Nyamhanga kuwa Usharika.

Baba Askofu, Mtaa wa Nyamhanga ulianza tarehe 11/08/2002 kwa juhudi za Waumini wa Mtaa huo kwa kushirikiana na Usharika wa Ipogolo.
Wakati Mtaa ulipoanza ulikuwa na Washarika 72, Washarika wamekuwa wakiongezeka siku hadi siku na kufikia Washarika 1,180 hadi Mtaa ulipofikia kupewa hadhi ya Usharika Mwezi Januari, 2013.

Baba Askofu, kuanzishwa kwa Mtaa wa Nyamhanga ilitokana na Waumini wa Mtaa wa huo na wakazi wa eneo hili kutaka kusogezewa huduma ya Kiroho katika eneo lao, kutokana na kikwazo cha Korongo lililoko kati ya eneo la Nyamhanga na Usharika wa Ipogolo kujaa maji wakati wa masika, Waumini wa eneo la Nyamhanga ilikuwa tatizo kwao kuvuka Korongo hilo na kwenda Ipogolo kuhudhuria Ibada,

Baba Askofu, Usharika huu wa Nyamhanga utakaoufungua leo, umetokana na Usharika wa Ipogolo, Nyamhanga ukiwa Mtaa moja wapo wa Mitaa kumi na mbili (12) ya Usharika huo wa Ipogolo.

Usharika wa Nyamhanga una Mitaa saba (7), Waumini  1,180,  watu wazima ni Waumini  703, kati ya hao, Wanaume ni 266 , na Wanawake ni 439.
Watoto jumla yao ni 485, Wanaume ni 210, na Wanawake ni 275,

Baba Askofu, Usharika wa Nyamhanga una Mitaa Saba (7) kama nilivyokwisha eleza hapo awali, Mitaa hiyo ni:-
(1)  Mtaa wa Stesheni – Nyamhanga una waumini 528
(2)  Mtaa wa Kitwiru  - 174
(3)  Mtaa wa Kibwabwa - 125
(4)  Mtaa wa Lugala - 221
(5)  Mtaa wa Mseke - 65
(6)  Mtaa wa Mosi - 11
(7)  Mtaa wa Isimila – 56

Katika Mitaa hiyo Saba (7), Mitaa Mitatu (3) ni Mitaa ya Mission, Mitaa hiyo ni ifutatayo:-
(1)  Mtaa wa Mseke
(2)  Mtaa wa Mosi
(3)  Mtaa wa Isimila

Baba Askofu, Usharika huu Mpya wa Nyamhanga una Wachungaji Wawili:
(1)  Mchungaji Nuru Makweta – Ambae ni Mchungaji Kiongozi
(2)  Mchungaji Lunyiliko Muhile

Baba Askofu, ninakuahidi kuwa mimi na Mchungaji mwenzangu, tutashirikiana na Waumini wote katika kuifanya kazi ya BWANA katika eneo hili la Usharika huu.
Kufunguliwa kwa Usharika huu wa Nyamhanga, kutaimarisha kueneza neno la Mungu na huduma yake katika eneo hili.

Pili, ni wajibu wa Usharika huu, nikiwa na maana ya Viongozi, Wahudumu na Watenda kazi wote wa Usarika huu wa Nyamhanga kuitangaza Injili kwa watu wote.

Baba Askofu, Usharika wa Nyamhanga pia una Mipango Kazi Kama ifuatavyo:-
(1)  Kazi ya Kiroho:
Kazi kubwa iliyooko mbele yetu ni pamoja na;-
(a)  Kueneza neno la Mungu katika eneo la usharika wa Nyamhanga
(b) Kushirikiana na Viongozi, Wahudumu na Watenda kazi wote wa Usharika katika kuitangaza Injili kwa watu wote, ili waweze kuokolewa kwalo na kumtumikia Mungu.
(c)  Kufanya Uinjilisti wa nyumba kwa nyumba katika eneo hili la Usharika’
(d) Kuimasha na kuendeleza Sel – groups
(e)  Kuandaa semina za neno la Mungu
(f)    Kuandaa Mikutano ya Injili
(g) Kusomesha Wachungaji na Wainjilisti
(h)  Tuna Mipango ya Kutembelea Sharika mbalimbali katika Dayosisi ya Iringa na nje ya Dayosisi kwa kutumia kwaya za Usharika wetu, katika kueneza Injili na pia kujifunza kutoka kwao.
(i)   Kuimarisha huduma za Maombi.

Neno linasema,
                        “BWANA ASIPOIJENGA NYUMBA, WAIJENGAO WAFANYA
                          KAZI  BURE,
                          BWANA ASIPOULINDA MJI YEYE AULINDAYE AKESHA
                          BURE”

        (Zaburi 127: 1)


(2)  Kazi za Kiuchumi:
    Ili kazi ya Kiroho iweze kupata msukumo wa kwenda mbele, tuna Mipango Mkakati ya kazi za Kiuchumi kama ifuatavyo:-
(a)  Kujenga ukumbi
(b) Kujenga Shule ya watoto wadogo (Kindergarten)
(c)  Kujenga Hostel
(d) Kuendeleza Mradi wa upandaji Miti katika shamba lililopo Lugala
(e)  Tuna mpango wa kujenga Maduka ya Biashara kuzunguka eneo la Kanisa
(f)    Pia tuna Mpango wa ujenzi wa shule ya  Ufundi

Mipango hii yote ni endelevu ( Mipango ya muda mrefu).

Baba Askofu,
Mahali popote pale hapakosi changamoto:
Usharika wetu kwa kuwa ndiyo unaanza, tuna changamoto zifuatazo:-
(1)   Usharika una changamoto kubwa ya usafiri, hatuna chombo cha usafiri kwa
ajili ya kuifikia Mitaa yetu ambayo ipo mbali kutoka Makao makuu ya usharika, pamoja na kufanya shughuli zingine za kila siku.

(2)   Tuna upungufu wa Majengo kwa ajili ya ofisi za idara mbali mbali katika
Usharika wetu.

Baba Askofu,
Kwa heshima nakuomba,  karibu ufungue rasmi usharika wa Nyamhanga leo tarehe 12/05/2013.

“BWANA YESU ASIFIWE”

AMEN

NURU MAKWETA
MCHUNGAJI KIONGOZI – USHARIKA WA NYAMHANGA,
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment