Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Sunday, August 10, 2014

Bunge Maalumu siyo mhimili wa Dola


Bunge likiendelea 
Wakati huu ambao Bunge Maalumu la Katiba limeingia katika awamu ya pili ya kujadili na hatimaye kupitisha Rasimu ya Katiba mpya, tulitarajia kwamba wajumbe wake, wakiwamo viongozi wa Bunge hilo wangekuwa tayari wamepata uelewa wa kutosha kuhusu dhana ya Bunge Maalumu la Katiba.
Hii ni pamoja na kusoma na kuelewa vyema Sheria ya Mabadiliko ya Katiba na Rasimu ya Katiba Mpya iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Tulitarajia pia kwamba wajumbe wa Bunge hilo wangekuwa wamezielewa vyema hadidu za rejea ambazo ndiyo hasa ulikuwa msingi wa Tume katika kukusanya maoni ya wananchi na hatimaye kutengeneza Rasimu ya Katiba Mpya. Pamoja na hayo yote, tulitarajia kwamba uelewa wa mambo hayo ungelisaidia Bunge hilo kufahamu mipaka yake kama ilivyowekwa na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba. Lakini mkanganyiko uliopo hivi sasa miongoni mwa wajumbe wa Bunge hilo unaonyesha kwamba hawajawa na uelewa wa kutosha kuhusu masuala hayo muhimu, hasa kuhusu nafasi na mamlaka ya Bunge Maalumu la Katiba kwa mujibu wa Sura ya 83 ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2011.
Ipo dhana potofu miongoni mwa wajumbe wa Bunge hilo kwamba chombo hicho ni moja ya mihimili mikuu ya Dola na kinayo mamlaka kamili kama ilivyo kwa Bunge la Muungano. Ndiyo maana wajumbe wengi wanataka eti Bunge hilo litunge kanuni zitakazolipatia ‘meno ya kuuma’ na kuadhibu wananchi wanaolikosoa au vyombo vya habari vinavyochapisha au kutangaza habari za wananchi wanaolikosoa. Hii ina maana kwamba wajumbe wengi hawakufaidika na semina elekezi iliyofanyika mjini Dodoma kabla ya kuanza kwa awamu ya kwanza ya shughuli za Bunge hilo. Ndiyo maana pia hawajaweza kutambua kwamba Bunge Maalumu halina dhima ya kuisimamia Serikali na kutunga sheria. Katika majadiliano yoyote, hakuna jambo la hatari kama wahusika kujadili masuala wasiyoyaelewa, kama tunavyoshuhudia wajumbe wengi wakifanya bungeni humo.
Bahati nzuri Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya mwaka 2011 imeunda vyombo muhimu na kukipa kila chombo hadidu za rejea. Kila chombo kimewekewa utaratibu wa kazi na mamlaka yake ambayo pia yamewekewa mipaka. Ndiyo maana Tume ya Mabadiliko ya Katiba imekusanya tu maoni ya wananchi na kuandika Rasimu ya Katiba. Kazi ya kuijadili Rasimu na kupitisha Rasimu ya Katiba ni ya Bunge Maalumu, ambalo pia limewekewa mipaka ya kutoandika Rasimu mbadala au kubadili mfumo wa Rasimu ya Katiba iliyoandaliwa na Tume.
Mpangilio huo unaonyesha bayana kwamba madaraka ya Bunge Maalumu la Katiba siyo mapana kupita kiasi kama wajumbe wake wengi wanavyodhani, kutokana na ukweli kwamba mchakato wa kupata Katiba Mpya ulikuwa na ushirikishwaji mkubwa wa wananchi. Kwa maana hiyo, hoja zilizomo katika Rasimu ya Katiba ni za wananchi wenyewe, siyo za Tume.
Lengo hasa ni kuzuia Bunge Maalumu lisikwapue na kuteka madaraka ya wananchi, hivyo ushiriki wake katika mchakato huo ni kuboresha Rasimu ya Katiba na kuipitisha.
Bunge hilo litafanya vyema iwapo litatambua kwamba jukumu lake kuu ni kujadili na kupitisha matarajio ya wananchi na ndoto zao ambazo waliziwasilisha katika Bunge hilo kupitia Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment