Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Monday, July 1, 2013

Historia mpya yaandikwa leoTanzania

Rais wa Marekani, Barack Obama anatua nchini kwa ziara ya siku mbili ikiwa ni hatua yake ya mwisho ya ziara yake barani Afrika.
Dar es Salaam. Yametimia! Baada ya siku kadhaa za kusubiri kwa hamu, vitabu vya historia ya Tanzania vinaongezewa kumbukumbu wakati Rais wa Marekani, Barack Obama atakapowasili nchini leo mchana kwa ziara ya siku mbili. Ndege ya Air Force One itakayombeba  Obama na msafara wake itakanyaga ardhi ya Tanzania saa 8.40 mchana kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere ambako atapokelewa na mwenyeji wake, Rais Jakaya Kikwete.
 Obama ambaye anafuatana na mkewe Michelle na binti zake, Malia na Sasha, anatua Tanzania ikiwa ni sehemu yake ya mwisho ya ziara yake barani Afrika.
Anawasili Tanzania akitokea Afrika Kusini ambako alikwenda Ijumaa baada ya ziara yake ya Senegal.
Historia imetimia
Imepita miaka 50, tangu Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere alipotembelea Marekani, Julai 13, 1963 na kukutana rais wa nchi hiyo wakati huo, John F Kennedy na ziara hiyo inaaminika kuanzisha urafiki wa viongozi hao ambao umedumu hadi sasa. 
Ujio wa Rais Obama una maana na faida kubwa kwa Tanzania katika maeneo ukiangalia kihistoria, kisiasa, kidiplomasia na kiuchumi pia.
Ziara ya  Obama ni heshima kubwa kwa Tanzania na itaingia katika vitabu vya kihistoria kwani ana rekodi ya kuwa mtu mweusi wa kwanza kuchaguliwa kuongoza taifa la Marekani. Kuchaguliwa kwake (Obama), ambaye baba yake mzazi alikuwa na asili ya Kenya kuliashiria nuru mpya kwa siasa za Marekani kwani watu weusi wa taifa hilo kwa miaka mingi walikuwa wakipigania haki za kufaidika na fursa za kiuchumi na kisiasa katika taifa la Marekani.
Tanzania, kwa miaka mingi ilikuwa inaunga mkono harakati za watu weusi na ndiyo maana iliikuwa karibu na viongozi wa harakati za kupigania haki za watu weusi.
Mwalimu Julius Nyerere alikuwa karibu na Martin Luther King na mkewe Correta , ambao waliongoza harakati za mtu mweusi kujikomboa.Pia, viongozi wengine wa harakati hizo za mtu mweusi kutambuliwa kule Marekani, Jesse Jackson, Andrew Young na Malcolm X waliitembelea Tanzania mara nyingi.    Obama alipochaguliwa kushika nafasi hiyo mwaka 2008 alifurahiwa na wapenda amani kote duniani na hasa Waafrika kwani walimhesabu kuwa ni sehemu yao.
Kuja kwake leo ni heshima kubwa kwani Tanzania inakuwa nchi ya nne  Afrika kutembelewa na Obama baada ya Ghana mwaka 2009 na ziara yake ya hivi karibuni ya nchi za Senegal na Afrika Kusini.
Ukizingatia kuwa  Obama  ana miaka mitatu na nusu kabla ya kumaliza kipindi chake cha pili cha uongozi wake huenda ziara hii ndiyo ikawa ya mwisho kwake barani Afrika akiwa na wadhifa wa rais.Hata hivyo, Tanzania itabakia katika vitabu ya kihistoria kuwa ni kati ya nchi chache za Afrika zilizotembelewa na rais mweusi wa kwanza wa Marekani.
Kwa jumla, Tanzania iko juu katika vipaumbele vya Marekani kwa bara la Afrika kwani katika kipindi cha miaka 13 itatembelewa na marais watatu , Bill Clinton aliyekuja mwaka 2000 na George W. Bush 2008.
Kwa nini Obama anakuja Tanzania?
Ujio wake umekuwa gumzo kubwa miongoni mwa Watanzania huku mijadala ikiendelea katika mitandao ya kijamii, vijiweni na hata kada za wasomi na wachambuzi pia zinachambua ugeni huo.
Ziara hiyo ya Obama imetafsiriwa inatokana na Tanzania kuwa na rasilimali nyingi na hasa kugunduliwa kwa gesi na dalili za kuwapo mafuta kwenye sehemu mbalimbali za nchi hii. Pia, kuwepo kwa rasilimali za madini kama dhahabu, almasi na urani, ambayo ina manufaa makubwa kwa vinu vya nyuklia vya nchi hiyo, inaweza kuwa kichocheo cha ziara hiyo.
Ingawa, pia kuna sababu nyingine kama  hofu ya China kutawala uchumi wa dunia, nchi ambayo katika miaka ya karibuni imeibuka kuwa tishio katika uchumi wa dunia na inawekeza kwa kasi barani Afrika, pia ni sababu inayotajwa na wengi.
Hofu hiyo inaweza kuoanishwa na ujio wa Rais wa China, Xi Jinping, ambaye aliitembelea  Tanzania mwezi Machi mwaka huu.
Kumbuka, Tanzania ilikuwa nchi ya pili kutembelewa na kiongozi huyo  alipochaguliwa kuliongoza taifa hilo lenye idadi kubwa ya watu duniani.
Rais Jinping  aliahidi msaada kwenye miradi yenye thamani ya Dola 800 milioni baada ya kusaini mikataba 17 katika maeneo ya miradi na misaada kutoka China.
Akizungumza na waandishi wa habari hivi karibuni, Balozi wa Marekani, Alfonso Lenhardt alipinga dhana kuwa Obama anakuja kwa sababu ya rasilimali na kuwaonya Watanzania waondoe hofu kwa wageni kuiba rasilimali zao.
Pia, alisema Marekani haina hofu na China kutoa misaada na kuwekeza Tanzania lakini angependa kuona urafiki huo unawanufaisha Watanzania.
Balozi Lenhardt alitaja sababu za ujio wa kiongozi huyo Tanzania kuwa ni kutokana na Tanzania kuwa na utawala bora ukilinganisha na nchi nyingi kusini mwa Jangwa la Sahara.Alisema kuwa sababu nyingine inayofanya  Obama kuzuru Tanzania ni kutokana na jitihada za Serikali yake katika kutengeneza mazingira mazuri ya uwekezaji na kasi ya ukuaji wa uchumi.
“Rais Obama anakuja kuunga mkono juhudi za Watanzania katika kutengeneza mazuri ya uwekezaji lakini bila kusahau kuwa kasi ya ukuaji wa uchumi wa Tanzania umeivutia Serikali ya Marekani,” aliongeza Balozi Leinhardt.
Balozi huyo alieleza sababu nyingine inayomleta Obama kuwa ni kuisaidia Tanzania katika kuendeleza fursa mbalimbali za kujiletea maendeleo.
Balozi Lenhardt alisema kuwa Marekani ni kati ya inaongoza kwa kutoa misaada kwa Tanzania na mwaka 2012 pekee ilitoa Dola 750 milioni kupitia Shirika la Millenium Challenge (MCC) ikisaidia sekta za umeme, maji na miundo mbinu.
Alieleza pia kuwa Tanzania inaunga mkono jitihada za Serikali kujitosheleza kwa chakula ikifadhili Mkakati wa Kukuza Kilimo Kusini mwa Tanzania (SAGCOT).
Sababu nyingine ya ujio wa Obama ni kuhimiza haja ya bara la Afrika kutayarisha viongozi wa kizazi kijacho. Obama ameanzisha programu ya kuandaa viongozi wa kizazi inayotwa `Young African Leaders Initiative’ na Watanzania watatu, Modesta Lilian Mahiga, Masoud Salim Mohamed na Malula Hassan Nkanyemka walishiriki katika mpango huo na kukutana na kiongozi huyo mwaka 2010.
Balozi Maajar anena
Naye Balozi wa zamani wa Tanzania nchini Marekani, Mwanaidi Maajar alikaririwa na gazeti dada la The Citizen akisema uhusiano kati ya Marekani na Tanzania ni kwa misingi ya heshima.
Balozi Maajar alisema kuwa Serikali ya Marekani inaichukulia Tanzania kuwa nchi ya mfano kwa utawala bora barani Afrika na ndiyo maana inataka kuisaidia.
Alisema katika kipindi alichokuwa Marekani, hata Rais Obama alisema anataka kuona Tanzania ikipiga hatua kiuchumi kutokana na utawala bora. “Marekani inataka kuona Tanzania ikiwa mfano wa nchi ambazo zimeinuka kiuchumi kutokana na misaada yake,” aliongeza Balozi Maajar. 
Rais Obama awekewa ulinzi mkali
Makachero wapatao 300 wanatazamiwa kuwa nchini katika kipindi chote cha ziara yake nchini Tanzania.Pamoja na makachero pia manowari ya kivita imesogezwa karibu na pwani ya Tanzania, pia helikopta na ndege ziko tayari nchini kusaidia safari hiyo ya kihistoria.Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Dar es Salaam atakapotua  leo nao uko chini ya walinzi wa maofisa wa usalama wa nchi yake na wenzao wa Tanzania.
Wamepanga kufanya hata upekuzi wa mizigo kwa abiria watakaokuwa wanaingia kwenye uwanja huo. Pia, magari yapatayo 150 nayo yameingizwa nchini kwa ajili ya kusaidia safari hiyo katika kipindi chote Obama atakapokuwa nchini.
Barabara kufungwa Dar
Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Said Meck Sadiq amesema kuwa baadhi ya barabara za Jiji la Dar es Salaam zitafungwa leo na kesho wakati wa ugeni wa Rais Obama.
Akizungumza na waandishi wa habari jana, Sadiq alisema barabara ya Nyerere itafungwa kuanzia saa 6.30 mchana hadi saa 9.30.
Sadiq alisema barabara hiyo itafungwa katika muda huo ili kupisha msafara wa Rais Obama, ambaye atatua nchini saa 8.40 mchana.
Alisema msafara huo utapita Barabara ya Nyerere katika maeneo ya Kipawa, Jet Club, Vingunguti, Tazara, Kamata, Gerezani na maeneo ya posta ya zamani, Magogoni hadi Ikulu.
Pia aliagiza maofisa wa Serikali, sekta binafsi na watu wengine wasiokuwa na mahala maalumu pa kuegesha magari kwenye Barabara ya Samora kutokuyaingiza magari yao.
“Tukikuta gari liko sehemu isiyokuwa na maegesho basi litavutwa na kupelekwa Kituo cha Polisi,” alionya Sadiq.
Alisema kesho Obama atatembelea mitambo ya kufufua umeme ya Symbion iliyopo Ubungo kuanzia saa 4:00 asubuhi na barabara za Ali Hassan Mwinyi, Sam Nujoma na Morogoro zitafungwa kuanzia 3:00 hadi saa 5:00.
Alisema baada ya hapo msafara huo utatoka katika mitambo ya Symbio kwenda Uwanja wa Ndege kupitia katika Barabara za Mandela hadi Tazara kuingia Barabara ya Nyerere hadi Uwanja wa Ndege.
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment