Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Monday, August 11, 2014

Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata),mchakato wa Katiba usitishwe hadi Januari 2016


Mbunge wa Longido, Lekule Laizer akizungumza katika semina ya wabunge kwa ajili ya kuwajengea uwezo wa kushugulikia masuala ya wananchi.Semina hiyo iliandaliwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP) mjini Dodoma jana. Picha na Emmanuel Herman      
Na Waandishi Wetu, Mwananchi
Dodoma/Dar. Shinikizo la kutaka kusitishwa kwa Bunge Maalumu la Katiba limezidi kuongezeka baada ya Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata), kusema mchakato huo usitishwe hadi Januari 2016 ili kupisha Uchaguzi Mkuu wa mwakani.
Pendekezo la Jukata linafanana na msimamo wa baadhi ya wajumbe wa Bunge hilo na wananchi wengine wa kada mbalimbali sababu ikiwa kukosekana kwa maridhiano baina ya pande mbili zinazovutana katika Bunge Maalumu, hali ambayo Mwenyekiti wa Jukwaa hilo, Deus Kibamba amesema imesababisha mgawanyiko mkubwa katika nchi.
Hata hivyo, Katibu wa Bunge Maalumu la Katiba, Yahya Khamisi Hamad ameweka wazi kuwa Bunge hilo halitasitishwa kama wanavyoshinikiza Watanzania wengi kwa sababu uamuzi huo hautabadili msimamo wa CCM wala wapinzani katika suala la idadi ya serikali wanazotaka.
“Hatuwezi kubadili misimamo iliyopo hata kama tutasitisha Bunge. Tusitishe Bunge halafu tufanye kitu gani? Kama ni suala la kuzungumza na kuelewana kwa nini tusifanye sasa! Tujadiliane sasa kwa sababu msimamo wa CCM au watu wengine kuhusu wanachokiamini, kuubadili haitawezekana,” alisema Hamad.
Mgawanyiko
Akizungumza na waandishi wa habari mjini Dodoma, jana Kibamba alisema mgawanyiko huo ulianza pale yalipoibuka makundi kwa misingi ya kiitikadi za vyama na kundi la wajumbe wanaotokana na vyama vya siasa vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) waliposusia Bunge hilo.
“Kitendo cha Ukawa kushindwa kurejea bungeni ni pigo na kinaunyima mchakato huo uhalali wa kisiasa na kisheria kwani kwa upande wa Zanzibar tumegundua kuwa wanapungua wajumbe 16 ili kuwezesha kupitisha Rasimu ya Katiba,” alisema Kibamba.
Alisema nje ya sheria na kanuni, Jukata haioni ulazima wa kuendelea na Bunge hilo ilhali ikifahamika wazi kwamba Rasimu ya Katiba haitapata uungwaji mkono na wajumbe kutoka Zanzibar na kwamba kuendelea na mchakato huo ni matumizi mabaya ya fedha.
“Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, Samuel Sitta alisema eti anaamini kwamba Bunge likikaribia mwisho watakuwa wamepata idadi ya kutosha, sasa kama muda wote hawakuwahi kufanikiwa kuwashawishi, ni kitu gani kitawawezesha kupata akidi katika muda huo?” alihoji Kibamba.
Badala yake Kibamba alisema muda uliopo unapaswa kutumika kwa ajili ya maandalizi ya Uchaguzi Mkuu wa 2015, uchaguzi wa serikali za mitaa, uandikishaji wa wapiga kura katika mfumo mpya wa kielektroniki na utoaji wa Vitambulisho vya Taifa.
“Katiba Mpya ya kidemokrasia na ya viwango vya kimataifa alivyoviweka Rais Kakaya Kikwete, haiwezi kukamilika na kutumika kwenye Uchaguzi Mkuu wa 2015,” alisema Kibamba na kusisitiza kuwa hakuna njia nyingine ya kunusuru mchakato wa Katiba zaidi ya kuusitisha:
“Kwa hali ilivyo sasa huwezi kusema CCM ni wamoja, kuna watu wana mitazamo tofauti, wengine wanataka Bunge lisitishwe na wengine wanasema liendelee, lakini hata katika Kundi la Ukawa siyo wamoja maana wangekuwa wamoja tusingesikia kwamba wengine wapo hapa Dodoma.”
Wabunge CCM vipande viwili
Katika hatua nyingine, wabunge wa CCM katika Bunge la Muungano jana walivutana kuhusu hoja ya kusimamishwa kwa mchakato wa Katiba Mpya kutokana na wajumbe wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) kususia vikao.
Mvutano huo ulijitokeza katika semina ya wabunge wa kamati za Bunge hilo kuhusu Dhana ya Kusikiliza Maoni ya Wadau iliyoandaliwa na Bunge la Muungano kupitia mradi wake wa kuwawezesha wabunge (LSP), unaofadhiliwa na Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNDP).
Mvutano huo ulianza wakati Mbunge wa Longido, Michael Lekule Laizer aliposema mchakato wa Katiba Mpya umekuwa ni jambo gumu na unaelekea kushindikana na hivyo kupendekeza usimamishwe hadi hapo kutakapokuwa na mwafaka.
Alisema mchakato huo umekuwa ni vurugu na umekosa utashi mpaka wananchi wanashindwa kuelewa nini kinachoendelea: “Ni vyema kuusimamisha ili jambo hilo lianze pakiwapo mwafaka.”
Hata hivyo, Mbunge wa Viti Maalumu, Pudenciana Kikwembe alisema siyo kweli kwamba wajumbe wa Bunge hilo waliobakia bungeni wameshindwa kujadili na kukamilisha mchakato... “Sisi tunajadili na tutaendelea kujadili hadi tutafika mwisho hata kama Ukawa hawapo ndani (ya Bunge).”
Hali hiyo ilimfanya Mwenyekiti wa semina hiyo, William Ngeleja kuingilia kati na kuwataka wabunge wenye maoni kuhusu mjadala huo wayapeleke kwa Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta.
“Semina hii haihusiani na Bunge la Katiba, hapa tulipo wote ni wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano, kama kuna mtu ambaye ana maoni kuhusu Bunge Maalumu apeleke maoni yake kwa utaratibu wa kawaida,” alisema Ngeleja.
Hata hivyo, kauli ya Ngeleja haikufua dafu kwani Mbunge wa Nkasi Kaskazini, Ally Keissy alisimama na kuhoji: “Zimeundwa tume nyingi, Tume ya Shelukindo (William), Tume ya Jaji Nyalali (Francis) na Tume ya Jaji Warioba (Joseph), zimekwenda kuchukua maoni ya wadau maoni hayo yako wapi? Yameenda wapi?”
Alisema tume hizo zimepoteza fedha nyingi za Watanzania lakini maoni ya wadau hayajulikani yamepelekwa wapi. Mbunge wa Kwela, Iginas Malocha alisema kuna tatizo la maoni ya wananchi kuingiliwa na wanasiasa na kutopelekwa panapostahili... “Hii inasababishwa na kukosekana kwa uzalendo, uadilifu na ukweli.”
Imeandikwa na Neville Meena, Sharon Sauwa (Dodoma) na Fidelis Butahe (Dar).
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment