Writen by
sadataley
10:38 AM
-
0
Comments
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda akiwaeleza jambo wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba katika Viwanja vya Bunge hilo mjini Dodoma jana.
Na Neville Meena,Mwananchi
Dodoma. Wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba
watakuwapo mjini Dodoma kwa siku 90 kwa lengo la kukamilisha mjadala na
kupitisha Rasimu ya Katiba itakayokwenda kupigiwa kura na wananchi.
Siku hizo ni ongezeko la siku 30 zaidi katika siku
60 ambazo ziliongezwa na Rais Jakaya Kikwete Julai 28, mwaka huu na
kuchapishwa katika Gazeti la Serikali (GN) namba 254 ya Agosti 1, mwaka
huu.
Kwa kuongeza siku hizo, Bunge Maalumu linaweza
kutumia zaidi Sh15.5 bilioni kwa ajili ya kugharimia posho ya kujikimu
na ile ya vikao kwa wajumbe wake wote 628 bila kuhusisha gharama
nyingine kama za watumishi na huduma mbalimbali.
Katika gazeti hilo, Bunge Maalumu lilipaswa kuanza
jana, Agosti 5 na kumalizika Oktoba 4 lakini ratiba ya Bunge hilo
iliyotolewa jana inaonyesha kuwa litamalizika Oktoba 31.
Mwenyekiti wa Bunge Maalumu, Samuel Sitta alisema
siku zinazohesabiwa kwa ajili ya kazi za Bunge hilo ni za kazi yaani
Jumatatu hadi Ijumaa na kwamba Jumamosi na Jumapili siyo sehemu ya siku
60 zilizoongezwa na Rais.
Hata hivyo, Katibu Mkuu Kiongozi, Ombeni Sefue
alisema hakuwa na taarifa iwapo Rais Jakaya Kikwete alikuwa amefanya
mazungumzo na uongozi wa Bunge Maalumu kuhusu hoja ya siku za mwishoni
mwa wiki na kwamba tarehe ya mwisho anayoifahamu kwa Bunge hilo ni
Oktoba 4.
“Kwa kweli sifahamu kuhusu suala hilo, lakini kwa
kuwa Rais ndiye mwenye mamlaka kisheria, siwezi kufahamu kama uongozi wa
Bunge umewasiliana naye na kama wamefanya hivyo basi GN itabadilishwa
ili kukidhi matakwa ya mabadiliko hayo,” alisema.
Akizungumza katika Viwanja vya Bunge jana, Waziri
Mkuu, Mizengo Pinda alisema tayari Rais Kikwete alishatoa ruhusa ya
kuzingatiwa kwa siku za mapumziko na zile za mwishoni mwa wiki katika
ratiba ya sasa.
“Tulipokuwa tunashauriana kuhusu jambo hili,
tulipitiwa hatukuzingatia kwamba GN inaweka ukomo wa tarehe ya Bunge
Maalumu, lakini baadaye wakati tunaanza utekelezaji tumelibaini hilo kwa
hiyo tukasema litarekebishwa,” alisema Pinda na kuongeza:
“Jambo ambalo tumekubaliana ni kwamba kwa sababu
suala la kufanya mabadiliko kwenye GN liko kwenye uwezo wa waziri mwenye
dhamana, tutamwambia tu aweze kufanya marekebisho kadri ambavyo uongozi
wa Bunge Maalumu ulikubaliana na Mheshimiwa Rais.”
Sheria za kazi
Katibu wa Bunge Maalumu, Yahya Khamis Hamad
alisema taratibu zilikuwa zikiendelea kuwasiliana na watendaji
serikalini ili kurasimisha uamuzi huo ambao umezingatia sheria za kazi
na ile ya utumishi.
Kifungu cha 23 cha Sheria ya Kazi na Uhusiano Kazini Namba 8 ya
2006 kinaeleza kuwa mfanyakazi anapaswa kuwapo kazini kwa siku tano au
saa 45 kwa wiki, sheria ambayo inaongoza utendaji katika sekta ya umma
na ile ya binafsi.
“Ni kweli kwamba tunajenga hoja hiyo maana kwa
mujibu wa sheria za kazi na zile za utumishi, siku za kazi ni tano na
ndiyo maana hata mabadiliko ya kanuni yanayopendekezwa yanalenga
kubadili vipengele ambavyo awali vilikuwa vikielekeza Bunge kufanya kazi
Jumamosi kwa nusu siku,” alisema Hamad.
Katika azimio lake la Aprili 4, mwaka huu, Bunge
Maalumu liliipitisha Jumamosi kuwa moja ya siku zake za kazi kwa
kuongeza kipengele cha nne katika Kanuni ya 14.
Sehemu ya kanuni hiyo inasomekea: “Bunge Maalumu
kwa siku za Jumamosi litakutana kuanzia saa tatu asubuhi hadi saa saba
mchana…”.
Hata hivyo, jana Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuni,
Pandu Ameir Kificho aliitaja kanuni hiyo ya 14 (4) kuwa miongoni mwa
zilizorekebishwa ili kuiondoa Jumamosi katika siku zilizotajwa kuwa za
kazi.
Muda zaidi
Habari ambazo gazeti hili imezipata zinasema baada
ya Serikali kukubali kuzingatia matakwa ya sheria za kazi katika siku
za kuendesha Bunge Maalumu, kumekuwapo na hoja ya kutaka Bunge hilo
lifidiwe Jumamosi, Jumapili na siku za sikukuu zilizojitokeza.
Hoja nyingine ni ile inayotaka Bunge hilo lifidiwe
siku 21 ambazo zilitumika kwa ajili ya kuandaa kanuni kwa maelezo
kwamba Sheria ya Mabadiliko ya Katiba ya 2012 inaelekeza kwamba siku 70
zilikuwa kwa ajili ya kujadili Rasimu ya Katiba na siyo kufanya kazi
nyingine.
Ikiwa Serikali itaridhia hoja hiyo, basi Bunge
Maalumu linaweza kuongezewa siku zaidi ya 35 kwa mchanganuo wa siku 21
zilizotumika kutunga kanuni, siku 14 zikiwa siku mbili (Jumamosi na
Jumapili) kwa wiki saba na siku za mapumziko zinazotokana na sikukuu za
kitaifa.
Hamad alisema kumekuwapo kwa hoja za aina hiyo
lakini akasema ni mambo ambayo hajaingizwa katika mfumo rasmi wa
kutekelezwa kupitia ofisi yake.
“Kama unavyofahamu wataalamu wetu wa sheria
wamekuwa wakitushauri mambo mengi kuhusu suala la muda za uendeshaji wa
shughuli za Bunge hili, kwa hiyo hayo uliyoyasema pia ni miongoni mwa
hoja zinazozungumzwa lakini bado hatujafika huko,” alisema.
No comments
Post a Comment