Writen by 
                            sadataley
7:18 PM
                            - 
                            
0
                            Comments
                          
  
            
Waziri wa Fedha, Saada Mkuya akiteta jambo na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda
 katika moja ya Vikao vya Bunge mjini Dodoma. Picha ya Maktaba. 
            
Na Elias Msuya, MwananchiDar/Uswisi. Kuna njia tatu ambazo Serikali ya Tanzania ikiamua 
kuzitumia inaweza kurejesha mabilioni ya fedha zake ambazo zimefichwa 
nchini Uswisi na kwingineko duniani, Mwananchi limebaini.
Uchunguzi ulifanywa na gazeti hili nchini Tanzania
 na Uswisi unaonyesha kuwa, Mosi, Serikali inaweza kuharakisha kurejesha
 fedha hizo ikiwa itatumia vyombo vyake vya dola kama vile mahakama 
kutaka maelezo na majina ya walioweka fedha katika nchi husika.
Pili Tanzania inaweza kupata fedha zake ikiwa 
itajiunga na Taasisi iitwayo Organization of Economic Cooperation 
(OECD), ambayo imekuwa msaada mkubwa kwa wanachama wake kurejesha fedha 
ambazo zimekuwa zikihamishwa kwa njia ya ukwepaji wa kodi (transfer 
pricing), na tatu ni kujiunga ‘Global Forum on Transparence and 
Exchange’.
Taarifa ya 2012 ya Benki Kuu ya Uswisi (SNB) 
iliripoti kuwapo kwa Sh314 bilioni kutoka Tanzania, lakini katika 
taarifa yake ya mwaka jana, 2013 kiasi hicho kiliripotiwa kupungua na 
kufikia Sh291 bilioni.
Dk Mark Herkenrath ambaye ni Ofisa Programu wa 
Taasisi ya Alliance Sud inayojishughulisha na harakati za kupinga 
uwekaji wa fedha haramu nchini Uswisi, alimwambia mwandishi wa gazeti 
hili nchini humo kuwa Tanzania inaweza kuwasiliana na Serikali ya Uswisi
 ikiwa inahitaji taarifa zozote kuhusu fedha zake zilizofichwa nchini 
humo.
“Kama kuna ombi la kimataifa na likakubaliwa na 
mamlaka ya Uswisi, taarifa zinaweza kutolewa. Serikali zinazodai kuibiwa
 fedha zinapaswa kuomba zenyewe taarifa ili zipewe, lakini katika 
uhalisia hili halitokei. Ni sawa na kumwomba mwizi ajitaje mwenyewe,” 
Herkenrath na kuongeza:
“Kwa mfano kama kuna uchunguzi Tanzania ambao 
unahusisha watu na ushahidi ukapatikana, Uswisi iko tayari kusaidia. Ni 
kwa fedha zilizopatikana kwa njia haramu tu.”
Mkuu wa kikosi kazi cha kurejesha fedha na mali 
cha Uswisi, Pascale Baeriwyl akizungumza na mwandishi wa Mwananchi mjini
 Bern, alisema Tanzania inaweza kurejesha fedha zake kama Serikali 
itakuwa na nia ya dhati ya kufanya hivyo.
“Hadi sasa Uswisi imesharudisha Dola za Marekani 
1.8 bilioni kwenye nchi zilizotoka,” alisema Baeriwyl na kuongeza: 
“Zinaitwa fedha za watawala (potentate funds) ambazo huwekwa kwenye 
taasisi za nje za fedha. Uswisi inayo mikakati ya kuhakikisha kuwa fedha
 na mali haramu haziingizwi katika taasisi zake za fedha,” alisema.
Hata hivyo, Balozi Anne Lugon- Moulin ambaye ni 
mkuu wa kitengo kinachoshughulikia nchi zinazozungumza Kifaransa kusini 
mwa Jangwa la Sahara alisema, Uswisi peke yake haiwezekani kufanikisha 
urejeshwaji wa fedha kama Serikali ya Tanzania haitatoa ushirikiano wa 
kutosha.
“Uswisi peke yake haiwezi kufanikisha kazi hii 
kama Tanzania haitoi ushirikiano. Ndiyo maana tunafadhili taasisi 
zinazopambana na utoroshwaji wa fedha haramu na mashirika ya misaada 
ambayo pia yanafanya kazi Tanzania,” alisema Moulin.
No comments
Post a Comment