Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Thursday, July 31, 2014

Serikali ina njia tatu za kurejesha ‘mabilioni ya Uswisi’


Waziri wa Fedha, Saada Mkuya akiteta jambo na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda katika moja ya Vikao vya Bunge mjini Dodoma. Picha ya Maktaba. 
Na Elias Msuya, MwananchiDar/Uswisi. Kuna njia tatu ambazo Serikali ya Tanzania ikiamua kuzitumia inaweza kurejesha mabilioni ya fedha zake ambazo zimefichwa nchini Uswisi na kwingineko duniani, Mwananchi limebaini.
Uchunguzi ulifanywa na gazeti hili nchini Tanzania na Uswisi unaonyesha kuwa, Mosi, Serikali inaweza kuharakisha kurejesha fedha hizo ikiwa itatumia vyombo vyake vya dola kama vile mahakama kutaka maelezo na majina ya walioweka fedha katika nchi husika.
Pili Tanzania inaweza kupata fedha zake ikiwa itajiunga na Taasisi iitwayo Organization of Economic Cooperation (OECD), ambayo imekuwa msaada mkubwa kwa wanachama wake kurejesha fedha ambazo zimekuwa zikihamishwa kwa njia ya ukwepaji wa kodi (transfer pricing), na tatu ni kujiunga ‘Global Forum on Transparence and Exchange’.
Taarifa ya 2012 ya Benki Kuu ya Uswisi (SNB) iliripoti kuwapo kwa Sh314 bilioni kutoka Tanzania, lakini katika taarifa yake ya mwaka jana, 2013 kiasi hicho kiliripotiwa kupungua na kufikia Sh291 bilioni.
Dk Mark Herkenrath ambaye ni Ofisa Programu wa Taasisi ya Alliance Sud inayojishughulisha na harakati za kupinga uwekaji wa fedha haramu nchini Uswisi, alimwambia mwandishi wa gazeti hili nchini humo kuwa Tanzania inaweza kuwasiliana na Serikali ya Uswisi ikiwa inahitaji taarifa zozote kuhusu fedha zake zilizofichwa nchini humo.
“Kama kuna ombi la kimataifa na likakubaliwa na mamlaka ya Uswisi, taarifa zinaweza kutolewa. Serikali zinazodai kuibiwa fedha zinapaswa kuomba zenyewe taarifa ili zipewe, lakini katika uhalisia hili halitokei. Ni sawa na kumwomba mwizi ajitaje mwenyewe,” Herkenrath na kuongeza:
“Kwa mfano kama kuna uchunguzi Tanzania ambao unahusisha watu na ushahidi ukapatikana, Uswisi iko tayari kusaidia. Ni kwa fedha zilizopatikana kwa njia haramu tu.”
Mkuu wa kikosi kazi cha kurejesha fedha na mali cha Uswisi, Pascale Baeriwyl akizungumza na mwandishi wa Mwananchi mjini Bern, alisema Tanzania inaweza kurejesha fedha zake kama Serikali itakuwa na nia ya dhati ya kufanya hivyo.
“Hadi sasa Uswisi imesharudisha Dola za Marekani 1.8 bilioni kwenye nchi zilizotoka,” alisema Baeriwyl na kuongeza: “Zinaitwa fedha za watawala (potentate funds) ambazo huwekwa kwenye taasisi za nje za fedha. Uswisi inayo mikakati ya kuhakikisha kuwa fedha na mali haramu haziingizwi katika taasisi zake za fedha,” alisema.
Hata hivyo, Balozi Anne Lugon- Moulin ambaye ni mkuu wa kitengo kinachoshughulikia nchi zinazozungumza Kifaransa kusini mwa Jangwa la Sahara alisema, Uswisi peke yake haiwezekani kufanikisha urejeshwaji wa fedha kama Serikali ya Tanzania haitatoa ushirikiano wa kutosha.
“Uswisi peke yake haiwezi kufanikisha kazi hii kama Tanzania haitoi ushirikiano. Ndiyo maana tunafadhili taasisi zinazopambana na utoroshwaji wa fedha haramu na mashirika ya misaada ambayo pia yanafanya kazi Tanzania,” alisema Moulin.
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment