Writen by
sadataley
1:49 PM
-
0
Comments
Na Waandishi Wetu, Mwananchi
Dodoma. Waziri Mkuu mstaafu, John Malecela
amesema siku 60 zilizotengwa kukamilisha mchakato wa Katiba Mpya kabla
ya kupelekwa kwa wananchi hazitoshi kwa kazi hiyo.
Akizungumza na katika mahojiano maalumu mjini Dodoma hivi karibuni, Malecela alisema: “Watahitaji siku zaidi…
Nadhani kosa moja ambalo tumelifanya ni la kujaribu kuweka muda maalumu wa kupitisha Rasimu ya Katiba.
Hata hivyo, huu muda tuliouweka hatukuuweka
kutokana na uzoefu wa ama nchi fulani, maana tuangalie nchi zilizoandika
katiba zao, tuseme nchi fulani walichukua miezi fulani kwa hiyo sisi
itachukua siku fulani. Hebu angalia, kanuni tu zilichukua siku 40 na
katika hizi siku 40 walizungumza sura ya pili na sita tu.”
Bunge Maalumu la Katiba litaanza Agosti 5, mwaka
huu mjini Dodoma kwa siku 60 kukamilisha awamu ya pili ya mchakato huo
baada ya kumalizika awamu ya kwanza mwanzoni mwa mwaka huu.
Akizungumzia mchakato mzima wa Katiba Mpya
Malecela alisema: “Bado ninaamini inawezekana tukapata Katiba Mpya kama
tutakwenda na moyo wa kusema nipe nikupe na haya mambo ya watu kutoka
kwenye mazungumzo unajua mara nyingine tunaangalia hapa tu.
“Nimekwenda katika sehemu nyingine za dunia. Mfano
wa Jamhuri ya Ireland na Serikali ya Waingereza ilichukua miaka mingapi
wakae chini? Iliwachukua miaka mingi lakini walikaa chini wakazungumza
wakafikia mahali walipo sasa hivi hakuna mgogoro.
“Wewe ulifikiria Marekani katika siku hizi itakuwa
na ubalozi Iran? Lakini sasa hivi wanafikiria kufungua ubalozi Iran.
Kwa hiyo mimi nasema tufuate mifano ya nchi nyingine, tusikate tamaa
haraka.
Kuhusu hatua ya Umoja wa Katiba ya Wananchi,
kususia vikao vya Bunge hilo alisema: “Hawa wametoka naamini bado watu
wanaweza wakazungumza nao na nyie vyombo vya habari mkawasaidia
kuwatolea mifano mingi tu duniani na kumekuwa na migogoro mahali
pengine. “Chukua mfano wa Sudan Kusini miezi miwili, mitatu iliyopita
siyo walikuwa wakipigana, huyu Rais anasema yule ni mhaini na yule
akatoa vikwazo, mimi siji lazima hiki na hiki kifanyike lakini sasa hivi
wako wapi! Si wako wanazungumza na mimi nadhani wanaelekea kuunda
serikali ya maridhiano.
“Kwa hiyo sikati tamaa, bado nina hakika kwamba
wenzetu waliotoka bado kuna nafasi ya kuzungumza nao kwa kuwapa maelezo
na wao watakuwa na fikra zao.”
Alisema kila upande utatoa maoni yake na kufikia mwafaka na kuhakikisha Katiba Mpya inapatikana.
Kuhusu Tanzania kama inahitaji Katiba Mpya kwa
sasa, Malecela alisema: “Mimi hapo nadhani nitawakera kidogo kwa sababu
mawazo yangu yako vingine kabisa.
“Suala la Katiba mimi ambaye nimekuwa Makamu Mwenyekiti wa CCM
kwa miaka 15 na mara nyingi Katiba zilizokuja ama zimetokana na Tanu au
na CCM. Sasa Serikali ya CCM ilileta mapendekezo ya kutunga Katiba Mpya.
Nilionana na Tume na nilikaa nao kwa saa mbili kwa hiyo kama ni mawazo
yangu niliyatoa huko yote.
“Nafikiri tujaribu kuwa makini. Mradi tumefika
mahali tumekuwa na Bunge la Katiba sasa sisi sote hasa viongozi
tuliobaki hebu tuwe kama watu wanaoangalia mpira. “Unajua mpira unaona
mchezaji kachoka lakini unasema kimbiakimbia, kumbe mwezako nguvu
zimemwishia.
“Tukianza kusema maneno hapa katikati, mimi
nikisema watasema unaona hata Malecela kasema... Tuwaachie wenzetu wa
Katiba, hawa wajumbe wa Katiba, wakae wazungumze, tutaelewana tu!”
Aliwapongeza wajumbe wa Bunge la Katiba kwa
kuendesha Bunge bila kanuni lakini baadaye wakasimama na kujitengenezea
utaratibu wao.
“Mfano mdogo, Yanga na Simba unawafungia katika
chumba kimoja halafu unawaambia watengeneze sheria za mpira. Watafika
mahali fulani wakimuona mchezaji wa Yanga mrefu sana, Simba watasema
kwenye kanuni tuweke wachezaji wasizidi futi fulani. Hata hivyo,
walifikia mahali fulani wakakubaliana.
Imeandikwa na Frank Sanga, Habel Chidawali na Sharon Sauwa.
No comments
Post a Comment