Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Monday, July 14, 2014

Ujerumani - Mabingwa wa Dunia!


Wachezaji wa timu ya taifa ya Ujerumani wakishangilia na Kombe la Dunia mara baada ya kulitwaa kwa kuichapa Argentina bao 1-0 katika mechi ya fainali iliyochezwa jana kwenye Uwanja wa Maracana mjini Rio de Janeiro, Brazil. Picha na AFP      
Na Mwandishi Wetu/AFPRio de Janeiro, Brazil. Ujerumani ndiyo mabingwa wapya wa dunia baada ya kuichapa 1-0 Argentina katika mechi ya fainali ya Kombe la Dunia 2014, mchezo uliochezwa kwenye Uwanja wa Maracana mjini Rio de Janeiro, Brazil.
Shujaa wa Ujerumani katika mechi hiyo alikuwa ni kinda Mario Gotze, aliyefunga bao la ushindi dakika ya 113, akiunganisha vizuri krosi ya Andre Schurrle.
Hili ni taji la nne la ubingwa wa dunia kwa Ujerumani huku ikiwa imecheza mechi nane za fainali ya Kombe la Dunia. Kwa ushindi huo Ujerumani imekuwa timu ya kwanza ya Ulaya kutwaa ubingwa katika ardhi ya Amerika Kusini, huku Argentina ikishindwa kumaliza ukame wa miaka 28 wa kutwaa ubingwa wa dunia tangu ilipotwaa taji hilo 1986 ikiifunga Ujerumani ya Magharibi.
Mechi hii ya fainali ilikuwa kama marudio ya fainali za 1986 na 1990, ambazo zilizikutanisha Ujerumani na Argentina.
Katika mechi ya jana, Ujerumani waliianza kwa kasi na kupeleka mashambulizi katika lango la Argentina, lakini Argentina walikuwa mahiri kupeleka mashambulizi ya kushitukiza katika lango la Ujerumani.
Dakika ya 21, Gonzalo Higuain alikosa bao akiwa na kipa Manuer Neuer wa Ujerumani baada ya kupiga shuti kali ambalo lilitoka pembeni ya lango.
Krosi ya Ezequiel Lavezzi ilimkuta Higuian katika eneo la hatari dakika ya 30, ambaye aliuweka mpira nyavuni, lakini mwamuzi alikataa bao hilo kwani Higuian alikuwa ameotea.
Ujerumani walilazimika kufanya mabadiliko katika dakika ya 30, baada ya kuumia Kramer, na nafasi yake kuchukuliwa na Andre Schurrle, mabadiliko ambayo yalileta uhai kwa Ujerumani kwani dakika ya 45 Benedict Howedes alipiga kichwa mpira wa kona ambao uligonga mwamba wa goli.
Kipindi cha pili Argentina ilimtoa Lavezzi na nafasi yake kuchukuliwa na Sergio Aguero, hivyo kuanza kwa kasi na katika dakika ya 47 Lionel Messi alipata nafasi nzuri, lakini alipiga nje mpira akiwa amebaki na kipa Neuer.
Hata hivyo, katika kipindi hiki cha pili Ujerumani walionekana bora zaidi katika kuanzisha mashambulizi ya kushitukiza, lakini walishindwa kuipenya ngome imara ya Argentina.
Hadi dakika 90 zinamalizika hakuna timu iliyopata bao, hivyo mwamuzi kuongeza dakika 30. Beki wa kati wa Ujerumani, Jerome Boateng pamoja na mabeki wa Argentina, Ezequeil Garay na Martin Demichelis walifanya kazi kubwa katika safu za ulinzi za timu zao.
Mwanzoni mwa dakika hizo 30 za nyongeza, Ujerumani ilipata nafasi nzuri, lakini shuti kali la Schurrle lilipanguliwa na kipa wa Argentina, Sergio Romero, na Argentina walipata nafasi dakika ya 96, lakini Rodrigo Palacio alishindwa kuitumia.
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment