Latest News

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)

UNIVERSITY OF IRINGA (Formerly Tumaini University-Iringa)
CALL FOR MARCH INTAKE APPLICATION 2017/18
NOW OPEN!
DEADLINE 30/03/2018
CALL 0743 802 615, 0677 048 677Read More

menu

Thursday, May 8, 2014

CUF yaonya kauli za kuvunja Serikali ya Umoja Zanzibar


Mwenyekiti wa Chama cha wananchi (CUF), Profesa Ibrahim Lipumba akizungumza jijini Dar es Salaam jana. Picha na Raphael Lubava 
Na Joyce Mmasi, Mwananchi
Dar es Salaam. Baraza Kuu la Uongozi la Chama cha Wananchi (CUF), limelaani kauli ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana aliyoitoa katika mikutano yake Zanzibar na kusema kuwa ina lengo la kuvunja Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK).
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba alisema jana kuwa, kauli hizo zilizotolewa na viongozi wa CCM kuhusu SUK ni za kichochezi zinazopandikiza mbegu za chuki na vurugu inayoweza kusababisha maafa makubwa.
“Serikali ya Umoja wa Kitaifa inatokana na maoni ya Wazanzibari wote na imesaidia kuleta amani na utulivu Zanzibar…. kauli za kuchochea kuivunja zinapandikiza mbegu ya chuki na vurugu,” Profesa Lipumba aliwaambia waandishi wa habari.
Alisema Baraza Kuu pia limelaani kauli iliyotolewa na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd kuwa Mwakilishi wa Mji Mkongwe (CUF), Ismail Jussa siyo raia wa Zanzibar na kuiita kuwa ya kibaguzi yenye lengo la kupandikiza chuki dhidi ya Wazanzibar na Watanzania wenye asili ya Kiasia.
Wiki iliyopita, katika mkutano wa hadhara wa CCM ulioongozwa na Kinana kwenye Viwanja vya Kibandamaiti, Unguja, Mnadhimu wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar (BLW), Salmin Awadh Salmin alisema wawakilishi wa CCM wanajiandaa kuwasilisha hoja binafsi kwenye Baraza hilo ili kuwapa nafasi wananchi wahoji iwapo wanataka kuendelea na SUK au la.
Salmin alisema wajumbe hao wamefikia hatua hiyo kwa kuwa wanaona lengo na matumaini ya kuundwa kwake yamefutika na hayana dalili njema katika siku za usoni.
Katika mkutano huo, Kinana alinukuliwa akisema kuwa kwa miaka 20 tangu kuanzishwa mfumo wa vyama vingi, Katibu Mkuu wa CUF, Seif Shariff Hamad amekuwa akiwayumbisha Wazanzibari kutokana na tabia yake ya kubadilisha ajenda za kisiasa na kutikisa misingi ya umoja wa kitaifa nchini.
Alisema tabia ya kiongozi huyo imekuwa haifahamiki na haijulikani anatafuta jambo gani licha ya kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais katika Serikali ya Umoja wa Kitaifa iliyoundwa mwaka 2010 na CCM na CUF.
Msimamo wa CUF kuhusu Ukawa
Profesa Lipumba alisema CUF inawahakikishia Watanzania wote kuwa wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kutoka chama hicho hawatarudi katika Bunge Maalumu hadi pale litakapojadili na kuiboresha Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa katika Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
“Tutashirikiana na wajumbe wote wa Ukawa katika mapambano ya kudai Katiba ya wananchi, tunawaomba wananchi waunge mkono juhudi hizi za kupigania kuheshimika kwa maoni yao katika kupata Katiba Mpya,” alisema.
Alisema Baraza Kuu la Uongozi la CUF, limeupongeza Ukawa kwa uamuzi wa busara wa kujiondoa kwenye Bunge la Katiba kwa kile walichoeleza kuwa lilipoteza mwelekeo na wajumbe walio wengi wakifuata maelekezo ya CCM ya kuacha kujadili rasimu iliyokuwapo na kujadili mpya yenye mfumo mpya ambao haukupendekezwa na wananchi.

Aliongeza kuwa, CUF inatoa wito kwa viongozi waliounda Ukawa kuendeleza umoja huo na kufahamu kuwa wananchi wamepata moyo na hamasa mpya baada ya kuanzishwa kwa umoja huo na kwamba wasikubali kugawanywa na CCM.
“Baraza Kuu la CUF linampongeza Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni, Freeman Mbowe kwa ukomavu wa kisiasa aliouonyesha wa kuvunja kambi rasmi iliyokuwa ikiundwa na chama kimoja na sasa kuvishirikisha vyama vingine, kikiwamo CUF.”
Bunge la Bajeti
Profesa Lipumba alisema CUF kimebaini kuwa nidhamu ya bajeti imeendelea kuporomoka na kutolea mfano wa bajeti ya 2013-2014 kwamba haikutekelezeka kutokana na makadirio ya mapato kuonekana makubwa kuliko hali halisi ya ukusanyaji.
Alisema CUF inalaani utaratibu aliouita mbovu wa misamaha holela ya kodi ambayo husababisha upotevu wa fedha za Watanzania. Alisema kwa mwaka huu wa fedha, zaidi ya Sh2 trilioni zimepotea kutokana na misamaha hiyo.
« PREV
NEXT »

No comments

Post a Comment