Writen by 
                            sadataley
1:15 PM
                            - 
                            
0
                            Comments
                          
            
Mbunge Freeman Mbowe 
            
Na Waandishi Wetu, Mwananchi
Dodoma. Bunge jana liligeuka uwanja wa kurushiana makombora pale
 wabunge walipoumbuana kuhusu baadhi yao kudaiwa kuwa ombaomba katika 
Mfuko wa Pensheni kwa Wafanyakazi wa Serikali za Mitaa (LAPF).
Kuumbuana huko kuliegemea taarifa ya Mbunge wa 
Singida Mashariki (Chadema), Tundu Lissu kuwalipua baadhi ya mawaziri na
 wabunge kwa kuchota fedha katika mfuko huo.
Sakata hilo lilienda mbali zaidi baada ya Kiongozi
 wa Kambi Rasmi ya Upinzani, Freeman Mbowe kulipuliwa kuwa anadaiwa 
zaidi ya Sh1 bilioni na Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na 
tayari kuna hati ya kumkamata.
Hata hivyo, Mbowe alipoulizwa jana ofisini kwake 
bungeni alisema: “...Sina taarifa yoyote ya kukamatwa. Nipo hapa bungeni
 mbona sijakamatwa? Muulizeni aliyesema awaeleze imetolewa lini na 
nani,” alisema Mbowe.
Wabunge hao walianza kuumbuana baada ya Mbunge wa 
Mbinga Magharibi (CCM), John Komba kutaka mwongozo wa Spika, akidai 
Lissu alimtaja kuwa naye ni miongoni mwa wabunge waliochota fedha LAPF.
“Kati ya wabunge hao wanaofilisi mashirika ya 
umma, mimi sikumbuki wala sijui LAPF iko wapi wala ofisini kwa 
mkurugenzi wake wala kwa mfanyakazi wake na sijachukua fedha yoyote 
LAPF,” alisema.
Akionyesha kukerwa, Komba alisema anachokumbuka 
Mfuko wa Maendeleo wa Nyanza ambao ni wadau wa LAPF waliomba msaada wa 
kununua boti na walipewa Sh1.5 milioni... “Leo Lissu amekuja hapa 
anawadanganya watu kuwa mimi nimehusika kutoa mapesa LAPF, sijui huu ni 
wendawazimu ama nini?... Hizi ni siasa za majitaka kabisa naomba 
mwongozo wako.”
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, (Sera, 
Uratibu na Bunge), William Lukuvi alijibu hoja hiyo akisema wabunge 
kuomba katika mashirika hayo si jambo la ajabu na kwamba yeye mwenyewe 
aliomba kwa barua.
“Nilitaka kusema jambo hili si kubwa kiasi hiki kwa sababu fedha hizi zipo kwa ajili ya maendeleo...”
Hata hivyo, Lissu alipopewa fursa ya kujibu 
alipigilia msumari akisema wabunge ndio wenye jukumu la kusimamia mifuko
 hiyo na kwamba kama wanachukua fedha za mifuko hiyo wanaingia moja kwa 
moja katika mgongano wa kimasilahi.
Aidha, alisema LAPF kwenye fungu hilo la msaada 
kwa jamii inatoa kwa wabunge wa CCM pekee yake... “Kwa sababu wabunge 
waliopewa fedha na nyaraka zake zipo ni hao wanaopiga kelele kina Pindi 
Chana, Mwigulu Nchemba, wanaochukua fedha ni wa CCM tu.”
Alihoji kutumika kwa fedha za LAPF kununua jezi katika Jimbo la Chato linaloongozwa na Waziri wa Ujenzi, Dk John Magufuli.
Kwa habari zaidi ingia http://www.mwananchi.co.tz/habari/Kitaifa/Kuomba-fedha-LAPF--Wabunge-waumbuana/-/1597296/2327702/-/musv5z/-/index.html
Kwa habari zaidi ingia http://www.mwananchi.co.tz/habari/Kitaifa/Kuomba-fedha-LAPF--Wabunge-waumbuana/-/1597296/2327702/-/musv5z/-/index.html
 
 
 
 
 
 
 
No comments
Post a Comment