Spika Anne Makinda.PICHA|MAKTABA
Na Fidelis Butahe, Mwananchi
Dodoma. Moto wa mjadala wa bajeti kwa mwaka wa
fedha wa 2014/15 sasa unahamia katika kikao cha ndani cha mashauriano
kati ya Serikali na Kamati ya Bunge ya Bajeti kitakachofanyika kwa siku
sita.
Kikao hicho kilichoanza jana na kutarajiwa
kuendelea hadi Juni 11, kitajadili hoja zenye maslahi kwa taifa
zilizotolewa na wabunge wakati wa kujadili bajeti za wizara. Bajeti za
wizara zilianza kujadiliwa Mei 5 na kumalizika juzi jioni.
Spika Anne Makinda alitangaza jana kuanza kwa
kikao hicho na kufafanua kuwa kitawahusisha pia wenyekiti wa Kamati za
Kudumu za Bunge kwa ajili ya kutoa ufafanuzi wa masuala yanayozihusu
kamati zao.
Baadhi ya wizara ambazo wabunge walichachamaa
kutaka ziongezewe fedha ni pamoja na Wizara ya Maji, Afya na Ustawi wa
Jamii, Ujenzi, Uchukuzi, Kilimo Chakula na Ushirika, Nishati na Madini,
Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi.
“Bajeti ni Sh19 trilioni na katika kikao hicho
hakuna fedha itakayoongezeka. Kitakachofanyika ni kupunguza fedha katika
eneo fulani na kuipeleka eneo jingine,” alisema Spika Makinda.
Mvutano mkali unatarajiwa kuibuka katika kikao
hicho kutokana na wabunge wengi kuibana Serikali wakitaka iongeze fedha
kwa baadhi ya wizara katika Bajeti ya 2014/15 na kuhakikisha inaziba
upungufu wa fedha katika bajeti za baadhi ya wizara kwa mwaka 2013/14
unaomalizika Juni 30, mwaka huu.
Katika mjadala wa Wizara ya Afya, wabunge wengi,
hasa wanawake, waliibana Serikali kushinikiza iongeze fedha ili
kukabiliana na vifo vya akina mama na watoto.
Wizara hiyo imetengewa Sh622 bilioni ikiwa ni pungufu ya Sh131 bilioni kwa mwaka 2013/14 ambayo ilikuwa Sh753 bilioni.
Katika majibu yake, Serikali iliahidi kuongeza
fedha za wizara hiyo katika kikao hicho cha mashauriano huku ikitangaza
kutoa Sh12 bilioni kwa ajili ya kulipia deni la Bohari Kuu ya Dawa (MSD)
ambalo ni Sh89 bilioni na deni la matibabu nje ya nchi ambalo ni Sh21
bilioni.
Wizara ya Maji ni kati ya wizara ambazo wabunge
walichachamaa wakitaka Serikali iiongezee fedha ili iweze kukamilisha
miradi ya maji vijijini. Wizara ya Ujenzi nayo ni miongoni mwa wizara
zitakazojadiliwa.
No comments:
Post a Comment