Friday, May 2, 2014

Ni Atletico, Real Madrid fainali

London, England. Atletico Madrid imeitupa Chelsea nje ya mashindano baada ya kuichapa mabao 3-1 katika mechi ya marudiano ya nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kwenye Uwanja wa Stamford Bridge na hivyo kutinga fainali ya mashindano hayo.
Katika mechi ya kwanza iliyozikutanisha timu hizo wiki mbili zilizopita kwenye Uwanja wa Vicente Calderon mjini Madrid zilitoka suluhu 0-0.
Kwa ushindi huo, Atletico itacheza fainali dhidi ya Real Madrid na mechi hiyo ya fainali itapigwa Mei 24 kwenye Uwanja wa Da Luz mjini Lisbon, Ureno.
Real Madrid walifika fainali baada ya kuichapa Bayern Munich 4-0 katika mechi ya marudiano ya nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya juzi na hivyo kutinga fainali kwa jumla ya mabao 5-0 kwa sababu katika mechi ya kwanza wiki moja iliyopita walishinda 1-0.
Katika mechi ya jana, Chelsea walitawala mwanzoni mwa kipindi cha kwanza na kupata bao katika dakika ya 39 ambalo lilifungwa na Fernando Torres, lakini halikudumu muda mrefu kwani Atletico walisawazisha bao katika dakika ya 44 mfungaji akiwa Adrian Lopez.
Kipindi cha pili Atletico walimiliki zaidi mpira na kufanya mashambulizi katika lango la Chelsea na kupata penalti katika dakika ya 60 ambayo ilifungwa na Diego Costa baada ya Eto’o kumwangusha Costa katika eneo la hatari.
Bao hilo liliwatoa Chelsea mchezoni kwani walijikuta wakifungwa bao zuri la tatu katika dakika ya 72 ambalo lilifungwa na Arda Turan baada ya wachezaji wa Atletico kupasiana vizuri.

No comments:

Post a Comment